Baada ya kupambana kuitafuta tiketi ya kushiriki Michuano ya Barani Ulaya (UEFA) msimu ujao. Sasa Manchester United wanaelekea kwenye michezo ya mwisho kwenye kindumbwe ndumbwe cha kombe la Europa.

Manchester United walimaliza msimu wa Ligi Kuu ya England (EPL) bila kupoteza mchezo tangu Februari huku wakimaliza kwenye nafasi ya 3 katika msimamo wa ligi hiyo.

Meneja wa Mashetani hao Wekundi wa Old Trafford Ole Gunnar Solskjaer ambaye alikuwa na wakati mgumu katika kupanga kikosi imara, alitumia kikosi kimoja kwa michezo 5 ya mwisho na hivyo wachezaji hao kuchoka sana kutokana na muda mfupi waliotumia kati ya mchezo na mchezo.

Kuelekea katika hatua ya mtoano michuano ya Europa, Solskjaer anakila sababu ya kuwatumia wachezaji ambao hawajatumika sana katika michezo ya Ligi Kuu ya England (EPL). Lengo likiwa ni kuwapumzisha baadhi ya nyota wake na kuwapatia nafasi wachezaji wengine.

Daniel James, Odion Ighalo, Juan Mata, Scott McTominay, Fred, Lingard, Andreas Pereira na Sergio Romero ni kati ya wachezaji ambao Ole Gunnar Solskjaer amekuwa akiwatumia sana kwenye michuano ya Europa ikilinganishwa na EPL.

Japokuwa McTominay na Fred walipata nafasi ya kuonesha uwezo wao kwenye michezo ya EPL, ujio wa Bruno Fernandez na kurejea kwa Paul Pogba ambaye alikuwa majeruhi, kumewafanya wachezaji hao [McTominay na Fred] kukaa benchi kwa muda.

Kutokana na muda wa kuanza kwa msimu mpya wa EPL kuwa karibu sana (Septemba 12), ni dhahiri kwamba vilabu vinavyoshiriki michuano ya ulaya (Ligi Ya Mabingwa UCL na Europa League EL, vinakila sababu ya kufanya mabadiliko ya vikosi vyao katika michuano hiyo.

Solskjaer anafaida ya kuwa na kikosi kipana chenye wachezaji wenye uzoefu na ambao wameshatumika zaidi kwenye michuano hiyo. Pia, uwepo wa vijana chipukizi kama James Garner, Tahit Chong, Laid na wengineo ni msaada mkubwa kwa Solskjaer na benchi la ufundi la Manchester United.

United wanarudi katika michuano hii wakikutana na LASK ambayo walipoteza kwa Man United [5-0]. Hii ni faida kwa United ambao ni kama wanakamilisha ratiba hii na kuangazia zaidi hatua ya robo fainali.

Vyombo vya habari mbalimbali nchini Uingereza viliripoti taarifa ya kuongezwa kwa muda kwa timu zinazoshiriki Michuano ya Ulaya. Endapo timu shiriki zitacheza mpaka hatua ya fainali – Agosti 21 (Europa), zitaongezewa muda wa siku 7 zaidi ya timu zingine kunako EPL kwa ajili ya mapumziko na kujiandaa kuanza msimu mpya.

Wakati Manchester United na Wolverhampton Wanders wakipambana na Europa nchini Ujerumani. Manchester City na Chelsea wao watakuwa wanacheza michuano ya UEFA itayochezwa Ureno. City wakivaana na Real Madrid, wakati Chelsea wakikipiga dhidi ya FC Bayern Munich.

Willian, Chelsea bado ngoma mbichi
Pedro afanyiwa upasuaji