Mshauri wa Usalama wa Taifa wa Marekani, John Bolton amesema kuwa nchi hiyo inahitaji mabadiliko ya haraka zaidi kuhusu sera zake barani Afrika ili kuweza kukabiliana na kuongezeka kwa ushawishi wa kifedha na kisiasa wa China na Urusi barani humo.

Amesema kuwa misaada yote ya Marekani kwenda Afrika ambayo ni jumla ya dola bilioni 8 katika kila mwaka wa fedha kwa vipindi viwili vilivyopita inafanyiwa tathmini ya mwisho.

“Kulingana na mtazamo wetu mpya, kila uamuzi tunaofanya, kila sera tunayofuata na kila dola ya msaada tunayotumia itakuwa na kipaumbele cha Marekani kwanza katika eneo husika,”amesema Bolton

Wakati Bolton akizungumzia sera ya utawala kwa Afrika, waziri wa ulinzi wa Marekani, Jim Mattis yeye ametangaza kuwa nchi hiyo haitasaidia tume za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa ambazo hazionyeshi maendeleo wala mafanikio.

Aidha, Marekani ni mfadhili mkubwa wa operesheni za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa ambapo inatoa takribani theluthi moja ya bajeti yake ya dola bilioni 6.7 kwa mwaka wa fedha ulioanza Julai mosi 2018 hadi June 30 mwaka 2019.

Mwaka jana balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Nikki Haley aliongoza juhudi za utawala kupunguza bajeti nzima ya ulinzi wa amani, ambapo Umoja wa Mataifa ulikubali kupunguza bajeti hiyo kwa dola milioni 500.

Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wanaonya dhidi ya Marekani kuliangalia Bara la Afrika katika mtazamo wa kiushindani kwani thamani ya Marekani barani Afrika itashuka.

Simba wajipa matumaini ya ushindi
Tanzania yafungua ofisi ndogo za Ubalozi HongKong nchini China