Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni amesema, mbinu ya askari wa usalama barabarani kujificha kwa ajili ya kubaini madereva wanaovunja sheria za usalama barabarani imechangia kupunguza ajali kwa asilimia 43.

Mhandisi Masauni amesema hayo leo tarehe 6 Mei 2019 bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge Viti Maalumu, Mariamu Sabaha aliyehoji hatua zilizochukuliwa na serikali kwa trafiki wanaotumia njia hiyo akidai kwamba imesababisha baadhi ya ajali.

“Mkakati wa kupunguza ajali za barabarani ulisaidia kupunguza ajali zaidi ya asilimia 40.Mkakati huo ulihusisha mbinu mbalimbali zenye lengo la kulazimisha dereva kufuata sheria, serikali haina ushahidi wa ajali zilizosababishwa na trafiki kujificha.” amesema Masauni.

Masauni amesema ili kutekeleza majukumu yao, huanzisha mbinu mbalimbali ambazo hazivunji sheria katika kudhibiti madereva wanaokiuka sheria na kusababisha ajali.

Ameongezea tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani, kulikuwepo na ajali za mara kwa mara ambazo nyingi zilizosabaishwa uzembe wa baadhi ya madereva wasiofuata sheria za barabarani hivyo askari wa usalama barabarani walibuni njia hiyo ya kujificha ili kubaini madereva wanaokiuka sheria hizo.

Amesema, Trafiki wana nia njema wanapotumia njia ya kujificha kubaini madereva wasiowaaminifu, na wala hawana dhamira ya kubughudhi wananchi, na kwamba kama njia hiyo ina usumbufu serikali itaangalia namna ya kuondoa.

Kanisa katoliki lasimamisha ibada zake
Video: Kopa Fasta yaneemesha wasanii Mwenge