Chama cha Upinzani cha Labour nchini Uingereza kimevunja mazungumzo ya wiki sita ya Brexit ya kupata muafaka na waziri mkuu, Theresa May na kulalamika kuwa mamlaka yake yako ukingoni na utawala wake unakaribia mwisho.

Kiongozi wa chama cha Labour nchini humo, Jeremy Corbyn amesema kuwa mpasuko kati yao hauwezi kuzibwa na ile hali ya kujiamini haipo tena kwamba mrithi wake ataendelea na maridhiano yoyote yanayoweza kupatikana.

“Ongezeko  la udhaifu na kutokuwa thabiti kwa serikali yako kuna maana hakutakuwa na imani katika kulinda chochote kinachoweza kukubaliwa baina yetu,” amesema Corbyn

Amesema kuwa chama cha Labour kitaendelea kupinga makubaliano yaliyofikiwa na serikali kama yalivyo hivi sasa kuhusiana na Uingereza kujitoa katika umoja wa Ulaya.

Aidha, wabunge kwa mara tatu mfulilizo waliyakataa makubaliano yaliyofikiwa na May pamoja na Umoja wa Ulaya na kumlazimisha kuchelewesha tarehe ya  Brexit  mara  mbili huku wakikinyooshea kidole chama cha Labour.

Bunge linatarajiwa kupiga kura kwa mara ya nne mapema mwezi Juni kuhusiana na masharti ya Uingereza kujitoa kutoka Umoja wa Ulaya.

Hata hivyo, kuvunjika kwa mazungumzo hayo kumekuja siku moja baada ya May kukubali kuweka muda maalumu kwa ajili ya kuachia wadhifa wa uwaziri mkuu kufuatia kura ya kujitoa kutoka  Umoja wa Ulaya bungeni.

 

UWT Njombe waanza maandalizi ya Uchaguzi
Membe: Rostam wewe ni mwenzetu, wote ni watoto wa kambo