Kiungo wa zamani wa klabu ya Young Africans Ally Mayayi Tembele ameutaka uongozi wa klabu hiyo kuhakikisha wanafanya usajili wa washambuliaji mahiri wa pembeni, wakati wanafikiria kuboresha safu ya ushambuliaji wa kati.

Mayayi ambaye kwa sasa ni mchambuzi wa soka, amewashauri viongozi wa klabu hiyo kongwe hapa nchini, baada ya kuona kuna mapungufu makubwa kwenye nafasi hiyo katika kikosi cha Young Africans kwa msimu huu wa 2019-20.

Amesema msimu huu amefuatlia kwa kina na kujiridhisha kwamba, kikosi cha Young Africans kimekua na mapungufu makubwa kwa kukosa aina ya washambuliaji wa pembeni, kama ilivyokua miaka ya nyuma.

“Ukiangalia soka la kikosi cha Young Africans mara nyingi wamekuwa wakitumia mawinga kufanya mashambulizi, tangu alipoondoka Msuva, timu haijapata mbadala wake,”

“Ni vyema kipindi hiki ambacho wameanza kusaka wachezaji wa kuwasajili kwa ajili ya msimu ujao wa ligi wakajaribu kusajili mawinga wa kulia na kushoto ambao wana kasi kama ilivyokuwa wakati wa Msuva.” Amesema Mayayi ambaye amewahi kuwe mjumbe wa kamati ya ufundi ya klabu hiyo.

Katika hatua nyingine mdau huyo wa soka la Bongo pia ameshauri usajili uzingatie upande wa walinzi pembeni ili kuwaongezea nguvu waliopo kwa sasa.

“Upande wa safu ya ulinzi hakuna matatizo makubwa lakini ni vyema wakaongeza nguvu. Kwani baadhi ya wachezaji kama Kelvin Yondani, Juma Abdul hawana ubora waliokuwa nao miaka minne iliyopita”

“Walinda mlango sidhani kama wanahitaji kwenye usajili ujao, naamini waliopo kikosini wanatosha, muhimu waongeze umakini tu ili wafanye vizuri zaidi”

Ngorongoro: wanafunzi 12 wapewa ujauzito
Diamond kugusa kaya 500 nchi nzima, ''Anayelipa kodi milioni kayataka mwenyewe''