Wakati shirikisho la soka nchini TFF likiendelea kutangaza kuwa na uhakika wa kumtumia mshambuliaji wa klabu ya KRC Genk ya Ubelgiji Mbwana Samatta katika mchezo wa Taifa Stars, imeelezwa kuwa mshambuliaji huyo ambaye ni nahodha wa kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, atakaa nje kwa majuma sita akiuguza majeraha ya goti.

TFF kupitia kwa afisa habari wake Alfred Lucas leo mchana ameviambia vyombo vya habari kuwa, mshambuliaji huyo atajiunga na kikosi cha Taifa Stars mjini Benin tayari kwa mchezo wa kimataifa wa kirafiki utakaochezwa mwishoni mwa juma hili, lakini taarifa za kuumia kwa Samatta zinadhihirisha hatokua sehemu ya kikosi Tanzania.

Samatta aliumia goti mwishoni mwa juma lililopita wakati akiichezea Genk dhidi ya Lokeren na kulazimika kutolewa nje katika dakika ya 40.

Samatta ameonekana kupata maumivu katika goti lake katika misuli na mifupa miepesi ambayo kitaalamu inajulikana kama Meniscus.

Azam FC yavunja mkataba na Yahaya Mohammed
Safari ya Said Ndemla yasogezwa mbele