Serikali imetoa wito kwa wanasiasa kutotumia masuala ya Muungano katika masuala yao ya kisisa kwani watu wa pande mbili za Muungano hawawezi kufarakana kwa sababu ya umiliki wa eneo.

Akijibu swali la Mhe. Jaku Hashim Ayoub lililohusu umiliki wa kisiwa cha Latham (Fungu Mbarak), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) January Makamba amesema kuwa katika orodha ya changamoto 14 za Muungano zilizoshughulikiwa na zinazoendelea kushughulikiwa hakuna suala lolote linalohusu umiliki wa eneo.

Waziri Makamba  amesema hakuna mgogoro wowote unao husu umiliki wa eneo lolote baina ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Jamhuri ya Muungano  wa Tanzania kwa kuwa tafsiri na suala zima la mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar limewekwa wazi katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano na Katiba ya Zanzibar.

Waziri Makamba amesema kuwa kuhusu suala la mafuta na gesi hakuna mgogoro wowote kwani leseni za utafutaji wa mafuta zilitolewa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) katika eneo hilo kwa mujibu wa Sheria ya Utafutaji Mafuta na Gesi Asilia ya mwaka 1980.

“Hakuna mgogoro wowote wa mafuta na gesi baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, huko nyuma leseni za utafutaji mafuta zilitolewa na TPDC  katika eneo hilo kwa mujibu wa Sheria ya utafutaji mafuta na gesi asilia,” amefafanua Waziri Makamba.

Serikali Yaunda Timu ya Wataalamu wa Kutatua Migogoro ya Ardhi Nchini
TACAIDS Imeyataka Mashirika na Taasisi Kuepuka Kujiingiza Kwenye Unaharakati Kinyume cha Sheria