Siku moja baada serikali kutangaza uamuzi wa kulifungia maisha gazeti la Mawio, Mhariri Mkuu wa gazeti hilo ambaye pia ni Mkurugenzi wa kampuni ya Victoria Media inayolimiliki gazeti hilo, Simon Mkina ameeleza jinsi walivyopokea taarifa hizo.

Mkina alieleza kuwa ingawa wamekuwa wakisikia habari za kufutwa kwa gazeti lao kweye vyombo vya habari ikiwemo mitandao ya kijamii, bado hawajapata taarifa rasmi kutoka serikalini kuhusu uamuzi huo ili wajue hatua watakazoweza kuchukua.

“Sisi ndio waathirika wa wakubwa wa taarifa hii. Kinachotushangaza ni kuwa hadi sasa hatujapata barua yoyote ya serikali kuhusu jambo hili. Na sisi tumemsikia Waziri Nape akitangaza kutufuta na kwakweli tumeshtushwa sana,” alisema Mkina.

Aliongeza kuwa uongozi wa kampuni hiyo umepanga kukaa na kufikiria hatua sahihi za kuchukua kutokana na uamuzi huo.

Kadhalika, Mkina alieleza kuwa serikali inapaswa kuwapa taarifa ya maandishi kuhusu sababu zilizopelekea kufutwa kwa gazeti lao na habari iliyosababisha wafutwe. Alisema wanashindwa kufahamu ni habari gani ilisababisha wafutwe kwa kuwa walikuwa wakipokea barua ya kujieleza karibia kila baada ya wiki mbili kuhusu habari walizokuwa wanaziandika.

Alisema kuna tofauti ya sababu zinazopelekea kufutwa na sababu zinazopelekea kufungiwa hivyo wanataka kujua ni habari gani zilizopelekea wafutwa.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Michezo na Sanaa, Nape Nnauye alisema kuwa gazeti hilo lilifutwa kutokana na kuandika habari za uchochezi na zenye utata na kwamba wamiliki wa gazeti hilo wamekuwa wakionywa na serikali tangu mwaka 2013 lakini hata majibu yao yalikuwa ya kiburi na dharau.

Mawio limefungiwa maisha kuanzia Januari 15 mwaka huu.

 

 

 

 

Diamond afichua kuwa ana mtoto mwingine tofauti na 'Tiffah'
Simba Waachana Na Wazungu, Kufanya Kazi Na Mzanzibar