Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella amesema hadi kufikia muda huu idadi ya waliofariki dunia katika ajali iliyotokea jana ya kivuko cha MV Nyerere kuzama yafikia 94 huku zoezi la uokoaji likiwa bado linaendelea ambapo watu 40 wameokolewa wakiwa bado hai.

Idadi hiyo imefikiwa baada ya miili 50 kupatikana leo mara baada ya zoezi la uokoaji kuendelea na miili 44 kupatikana jana.

Kivuko hiko kilichokuwa kinafanya safari zake kati ya Bugorola na Ukara kilizama jana majira ya saa nane mchana, mita 50 kabla ya kutia nanga kisiwa cha Ukara.

Ajali hiyo inadaiwa kusababishwa na idadi kubwa ya abiria waliobebwa kulingana na uwezo wa meli hiyo ambayo uwezo wake ni kubeba abiria 100.

DC Ukerewe amesema kivuko kilikuwa kimebeba zaidi ya abiria 400, kilivyokaribia kufika kupiga nanga nahodha akapunguza spidi hivyo abiria wakakimbilia upande wa kutokea ili wawahi kutoka, kivuko kikazidiwa uzito na kupinduka.

Aidha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli ametuma salamu za rambirambi na pole kwa wote waliopoteza jamaa zao na wote walionusurika kupona haraka, na ameomba watanzania waendelee kutulia katika kipindi hiki ambacho harakati za uokoaji zinaendelea.

Wawili waenguliwa uchaguzi klabu ya simba
Video: Tido amtaja JK Kortini, Lissu ataja mbinu mpya za ushindi