Mshambuliaji wa Simba Miraji Athumani amesema amepona majeraha yaliyomuweka nje kwa zaidi ya miezi minne, hivyo yupo tayari kurejea kikosini wakati wowote pindi ligi itakaporejea.

Miraji maarufu kama “Sheva” aliweka bayana hukusu maendeleo ya hali yake kiafya, alipohojiwa na mashabiki wa Simba kwenye kipindi cha ChatNa, kinachoendeshwa kupitia kurasa za mitandao ya kijamii za klabu ya Simba.

Sheva alisema tayari ameanza mazoezi na anajihisi kuwa sawa, kutokana na kufuata ushauri wa kitabibu aliopewa.

“Namshukuru Mwenyezi Mungu nimepona kabisa na najisikia kuwa na afya njema na tayari nimeshaanza mazoezi mepesi,”

“Nilikuwa na wakati mgumu kipindi chote nilichokuwa sichezi kwani nilitamani nami niingie uwanjani lakini ndio hivyo isingewezekana kutokana na majeraha”

“Ninaendelea kufanya mazoezi ili nikirejea kikosini niweze kuendeleza pale nilipoishia”

Katika michezo kumi aliyocheza akiwa na Simba SC mwanzoni mwa msimu kabla ya kupata majeraha, Miraji alifunga mabao sita na kusababisha mabao mengine manne.

Sheva alipatwa na majeraha ya kifundo cha mguu mwanzoni mwa mwaka huu, na kwa muda mrefu alikua kwenye matibabu chini ya uangalizi wa klabu yake ya Simba SC.

 

Tanasha afunguka uhusiano ‘mgumu’ na Mama Diamond, sababu za kuachana
Muigizaji wa ‘Star Wars’ afariki dunia kwa Corona