Mshambuliaji Harry Kane huenda akawa sehemu ya kikosi cha Tottenham Hotspurs wakati watakapocheza dhidi ya Arsenal kwenye muendelezo wa Mshike Mshike wa Ligi kuu ya England, mwishoni mwa juma hili.

Kane alicheza dakika 90 za mchezo dhidi ya Chelsea mwishoni mwa juma lililopita huko Stamford Bridge, lakini kuna kuna mashaka kama atakuwa sawa kuelekea mpambano dhidi ya Arsenal ambao wanashikilia nafasi ya 14 kwenye msimamo wa ligi.

Taarifa za uhakika wa mshambuliaji huyo kutarajiwa kuwa sehemu ya kikosi cha Spurs mwishoni mwa juma hili, zimetolewa na meneja Jose Mourinho alipozungumza na waandishi wa habari kuelekea pambano wa Europa League leo Alhamis dhidi ya LASK.  

Jose Mourinho anaamini Harry Kane atashiriki kwenye mchezo dhidi ya Arsenal licha ya kuendelea kuuguza jeraha ambalo litamfanya mshambuliaji huyo asiwe sehemu ya kikosi cha Spurs kwenye mchezo wa Ligi ya Uropa na LASK.

Meneja huyo kutoka nchini Ureno pia akathibitisha wachezaji Erik Lamela, Carlos Vinicius na Sergio Reguilon kuwa majeruhi na hawatakuwepo kwenye mchezo wa leo dhidi ya LASK.

“Lamela ana jeraha kwa takribani wiki tatu au mwezi. Siamini kama anaweza kuwa na nafasi wikendi. Harry, Vinicius na Sergio – wanaweza kuwa na nafasi ya wikendi.”

Kuhusu Kane, “Sitakuambia hali ya jeraha lake [Kane]. Nadhani ana nafasi nzuri – ya kucheza dhidi ya Arsenal.”

“Sitaki kusema uwongo, sitaki kuficha chochote kuhusiana na kwamba atacheza au la? Nadhani atacheza. Hiyo ni hisia yangu kwamba atacheza.”

Kane ana mabao saba katika michezo 10 ya Ligi Kuu msimu huu na asilimia 66.67 ya nafasi zake kubwa, kwa data ya Opta.

Tottenham wanabaki kileleni mwa msimamo wa Ligi ya England kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa dhidi ya mabingwa watetezi Liverpool, licha ya kulazimisha sare ya bila kufungana dhidi Chelsea, mwishoni mwa juma lililopita.

Mwinyi apinga Corona kuwa kisingizio ukusanyaji kodi
Lwanga hadi Desemba 15