Aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Vunjo, Augustino Mrema (TLP), leo amekubali kufuta mashtaka aliyoyawasilisha katika Makakama Kuu Kanda ya Moshi akipinga matokeo ya ubunge yaliyompa ushindi James Mbatia (NCCR-Mageuzi).

Mrema ambaye alifungua kesi ya msingi katika mahakama hiyo akidai kuchezewa mchezo mchafu na Mbatia na timu yake katika siku ya uchaguzi ya Oktoba 25 mwaka jana jimboni humo, ameiomba mahakama hiyo kufuta kesi hiyo ikiwa ni siku chache baada ya kuanza kuwasilisha ushahidi wake.

Mbatia ambaye alifika katika mahakama hiyo, aliwaambia waandishi wa habari kuwa Mrema ametafakari ushahidi wake pamoja na mwenendo wa kesi na kuamua kufanya naye maridhiano.

“[Mrema] ameona muelekeo wa kesi sio mzuri kwa upande wake. Na alipoliona hilo kiutu uzima na baada ya kushauriwa na jashi alilotoka mahakamani wiki iliyopita, akaona hali inazidi kuwa mbaya kwa upande wake,” Mbatia aliwaambia waandishi wa habari.

Alisema kuwa wawili hao wameamua kufanya makubalino ili kumaliza kesi hiyo huku Mrema akiridhia kumrudishia Mbatia gharama za kesi hiyo.

“Makubaliano ya msingi ni kwamba ndugu Augustine Lyatonga Mrema amekanusha yale yote ambayo alileta mahakamani na ushahidi wake wote aliosema mahakamani na amekubali kurejesha gharama,” aliongeza Mbatia.

Mrema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa TLP, alifungua kesi hiyo kupinga ushindi wa Mbatia aliyepata kura 60,187 dhidi ya kura 16,617 alizopata Mrema katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika nchini Oktoba 25, mwaka 2015.

Mussa Kisoky: Tumebariki Adhabu Za Waliopanga Matokeo
Dayna Nyange aeleza alivyokuwa Rapa Mkali aliyelikuna sikio la Hermy B