Mwanafunzi wa kike wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha Pwani kilichoko Kaunti ya Kilifi nchini Kenya, jana alichomwa visu mara kadhaa na mwanafunzi mwenzake anayedaiwa kuwa alikuwa mpenzi wake.

Mwanafunzi huyo aliyetajwa kwa jina la Naomi Chepkemboi, alichomwa visu mara kadhaa kifuani na alikimbizwa katika hospitali ya Kaunti ya Kilifi anakoendelea kupatiwa matibabu.

Kwa mujibu wa Jeshi la polisi, mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kenyatta aliyetambulika kwa jina la Henry Kipkoech, ambaye alikuwa mpenzi wake anashikiliwa na jeshi hilo kwa tuhuma la kumchoma kisu Naomi.

Ripoti ya awali ya Polisi imeeleza kuwa Henry alifika kwenye nyumba ya Naomi jana asubuhi akiwa na begi lenye visu vitatu. Aliingia ndani na kufunga mlango kisha kuanza kumshambulia msichana huyo ambaye alipiga kelele za kuomba msaada. Wanafunzi wenzake ndio waliofanikiwa kumuokoa.

Mtuhumiwa huyo alikamatwa na kupelekwa kwenye kituo cha polisi cha Kilifi ambako anashikiliwa kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria, kwa mujibu wa Citizen.

Video: Ndugai na CAG ni zaidi ya vita, Spika amtaka CAG ajiuzulu
Viongozi wa Serikali ya Al-Bashir wakamatwa, wananchi wapewa makucha