Mwanafunzi wa darasa la saba mwenye umri wa miaka 15 katika shule ya msingi Rung’abure wilayani Serengeti amefungishwa ndoa ya kimila na mtoto mwenzake mwenye umri kama wake kwa mahari ya ng’ombe 10.

Tukio hilo lilitokea februari 15, na kuzua gumzo kwa wananchi, wanafunzi na watendaji wa serikali ambao wametaja kuwa ni kawaida kwa familia hiyo kuwakatisha masomo watoto na kuwaozesha.

Mwenyekiti wa kijiji cha Nyamerama, Sungura Matongo amekiri mwanafunzi huyo kumuoa binti mwenye miaka 15 anayedaiwa kumaliza darasa la saba katika shule ya msingi amani mwaka 2019.

“Hili suala ni kweli limefanyika na sherehe ilifanyika nyumbani kwa Nyamhanga, sisi hatujachukua hatua kwakuwa niliona la kawaida ” amesema Matongo.

Mwalimu mmoja wa shule ya msingi Rung’abure amesema mwanafunzi huyo, Januari alikuwa anahudhuria masomo vizuri laki kuanzia Februari mahudhurio yake yamekuwa mabaya baada ya kukabidhiwa majukumu ya ndoa.

Ofisa elimu kata , Marwa Seba amesema amesha waeleza walimu waandike barua kuhusu tukio hilo ziende ofisi ya mtendaji wa kijiji na kata ili zitumwe ofisi ya elimu.

Baba mzazi wa binti aliyeolewa, Risso Koroso amesema ” mimi nilishapokea ng’ombe wala sikufuatilia kujua umri wake na kama anasoma nilimuona kama mkubwa hivi”.

Mkuu wa wilaya hiyo Nurdin Babu ameliambia gazeti la Mwananchi kuwa ameshangazwa na tukio hilo na atahakikisha anafuatilia.

Kigwangalla aridhishwa matengenezo barabara Ngorongoro
Video: Hatima ya Tundu Lissu kesho, Mkapa 'ajimwambafai