Serikali imesema ni kinyume cha sheria kwa askari mgambo kuwanyanyasa Mama Lishe na wafanyabiashara wengine wadogo nchini.

Akijibu swali la Mhe. Zaynab Vulu (Viti Maalumu) alilotaka kujua kwanini Serikali isiandae mazingira mazuri ya kufanyia kazi wafanyabiashara hao, Naibu Waziri Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Mhe. Seleman Jaffo amesema kuwa askari mgambo wanapaswa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu bila kuwanyanyasa wala kuwadhulumu wakati wakiwaondoa katika maeneo yasiyoruhusiwa.

Naibu Waziri Jaffo aliongeza kuwa Serikali inatambua na kuthamini mchango wa wafanyabiashara hao walioko katika sekta isiyo rasmi katika kukuza kipato na ajira.

Aidha, Naibu Waziri Jaffo amesema kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kwa askari mgambo yeyote atakayebainika kujihusisha na vitendo vya kuwanyanyasa wafanyabiashara na Mama Lishe wanapotekeleza majukumu yao.

Mbali na hayo, Naibu Waziri amezikumbusha  Halmashauri zote nchini kutenga maeneo kwa ajili ya wafanyabiashara ndogo ndogo wakiwemo Mama Lishe karibu na maeneo walipo wateja wao.

Zaidi ya hayo Naibu Waziri huyo amewataka wafanyabiashara wadogo nchini kufanya biashara katika maeneo yaliyotengwa rasmi na Halmashauri na kuacha kufanya biashara hizo katika maeneo yasiyoruhusiwa

Video: Mfumuko wa bei za bidhaa wapungua kwa asilimia 4.9 mwezi Agosti
Waziri Lukuvi Awasilisha Mswaada Wa Sheria ya Uthamini, Usajili na Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi Nchini