Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai, amesema, Bunge litaendelea kuwatambua wabunge wote walioapishwa wakiwemo 20 kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), 19 wa Viti Maalum na mmoja aliyeshinda katika uchaguzi mkuu.

Ndugai amesema hayo leo Novemba 30 wakati akaiwaapisha wabunge wawili, Humphrey Polepole na Riziki Lulida kwenye viwanja vya Bunge, jijini Dodoma.

“Waliokuwa na wasiwasi kuhusu wale Wabunge 19 (Halima Mdee na wenzake) sijui kuna hili kuna hili, niwatoe wasiwasi wale ni Wabunge kamili, na wanahabari mkiwaandika muwaite waheshimiwa,” amesema Ndugai.

“ Watanzania tupige vita na tukatae ukandamazaji dhidi ya wanawake kwenye jamii yetu kwa kisingizio chochote, Mbowe ni rafiki yangu amesimama akaanza kuwatukana hadharani Wabunge hawa wanawake, ni aibu kuwatukana wanawake hadharani,” ameongeza Ndugai.

“Mbowe umesahau Mdee alivunjika mkono kwa ajili ya kukufuata magereza, Bulaya alipigwa akazimia amepelekwa Aga Khan kwa ajili yako Mbowe, Matiko amelazwa Segerea mara nyingi kwa ajili yako, mshahara wao kuwafukuza hadharani bila kuwasikiliza, haiwezekani,” amesema Ndugai.

Aidha, Spika Ndugai amesema hivi karibuni atawapanga wabunge katika kamati mbalimbali, baada ya Rais kuunda Baraza la Mawaziri.

Spika awaapisha Polepole, Lulida
Prof. Kabudi akutana na mabalozi wa China, Sweeden na Finland