Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA) nchini Tanzania limetangaza matokeo ya kidato cha sita ya mwaka 2019

Katika matokeo hayo yaliyotangazwa na Katibu Mtendaji wa Necta mjini Unguja visiwani Zanzibar, Dkt. Charles Msonde amesema kuwa ufaulu umeongezeka kutoka asilimia 97.58 mwaka 2018 hadi kufikia asilimia 98.32 mwaka 2019 ikiwa ni sawa na asilimia 0.74.

Dkt. Msonde amesema kuwa mtihani huo uliofanyika kati ya Mei 6 hadi 23 mwaka 2019, watahiniwa 91,298 walisajiliwa wakiwamo wasichana 37,948 sawa na asilimia 41.56 na wavulana 53,350 sawa na asilimia 58.44.

Amesema kati ya watahiniwa waliosajiliwa, watahiniwa wa shule walikuwa 80,216 na watahiniwa wa kujitegemea walikuwa ni 11, 082.

Aidha, amesema kuwa kati ya watahiniwa 91,298 waliosajiliwa kufanya mtihani, watahiniwa 90,001 sawa na asilimia 98.58 walifanya mtihani na watahiniwa 1,297 sawa na asilimia 1.42 hawakufanya mtihani huo kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za ugonjwa na utoro.

Vile vile ameongeza kuwa watahiniwa wa shule, kati ya watahiniwa 80,216 waliosajiliwa, watahiniwa 79,770 sawa na asilimia 99,44 walifanya mtihani ambapo wasichana walikuwa 33,883 sawa na asilimia 99.57 na wavulana 45,887 sawa asilimia 99.35. Watahiniwa 446 sawa na asilimia 0.56 hawakufanya mtihani.

Hata hivyo, ameongeza kuwa watahiniwa wa kujitegemea kati ya 11,082 waliosajiliwa, 10,231 sawa na asilimia 92.32 walifanya mtihani na watahiniwa 851 sawa na asilimia 7.68 hawakufanya.

“Jumla ya watahiniwa 88,069 sawa na asilimia 98.32 ya watahiniwa waliofanya mtihani wamefaulu,” amesema Msonde

Wimbo wa Beyonce wenye Kiswahili waiinua filamu ya 'The Lion King', usikilize hapa
Kigwangalla anena kuhusu sanamu, 'Acheni dhihaka'