Waziri wa Mambo ya Nje wa Nigeria, Geoffrey Onyeama amesema kuwa kutokana na vurugu zinazoendelea nchini Afrika Kusini dhidi ya wageni, shirika la Ndege la Air Peace limejitolea kuwasafirisha bure kuwapeleka makwao wale wote watakaotaka ili kujiepusha na kadhia hiyo.

Amesema kuwa mmliliki wa Shirika la Ndege la Air Peace yupo tayari kuwasafirisha bure wale wote watakaotaka kurejea nchini humo siku ya Ijumaa.

“Wote watakaotaka huduma hiyo wanashauriwa kuwasiliana na Ubalozi wa Nigeria jijini Pretoria na ofisi ndogo za ubalozi jijini Johannesburg kwa matayarisho muhimu,”imeeleza taarifa ya wizara hiyo.

Aidha, mashambulizi ya biashara zinazomilikiwa na wageni nchini Afrika Kusini zimepokelewa kwa hasira kali na Wanaigeria ambao wanahisi wanalengwa na kuonewa.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Nigeria, Geoffrey Onyeama aliwaambia waandishi wa habari siku ya Jumatano kuwa kulingana na taarifa zilizowafikia, hakuna raia wa Nigeria aliyepoteza maisha kwenye ghasia zinazoendelea.

Hata hivyo, amesema kuwa serikali inaangalia uwezekano wa kumrejesha nyumbani balozi wake kutoka Afrika Kusini na kudai fidia kwa biashara zote za raia wa nchi hiyo zilizoshambuliwa.

Nigeria imesusia kuhudhuria Mkutano wa Kimataifa wa Uchumi unaofanyika Afrika Kusini kutokana na ghasia zinazoendelea.

Serikali ya Nigeria tayari imeshatoa onyo kwa rai wake waliopo Afrika Kusini wakiwataka kutosafiri ama kuelekea kwenye maeneo ambayo ghasia hizo zimeshamiri mpaka pale hali itakapotengemaa.

Serikali yasitisha safari za ndege kwenda Afrika Kusini
TFF yawashukuru wadau wa Soka nchini