Kashfa zinazomkabili  aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu zimetua mikononi mwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwa ajili ya uchunguzi.

Nyalandu anadaiwa kutumia ofisi vibaya na kuisababishia serikali hasara ya shilingi bilioni 32, katika kipindi cha miaka miwili alichoongoza wizara hiyo kuanzia mwaka 2014 hadi 2015.

Aidha, uchunguzi huo umejiri zikiwa zimepita siku 21 tangu Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamis Kigwangalla kulieleza bunge kuhusu kashfa tatu za ubadhirifu zinazomkabili Lazaro Nyalandu.

Katika mkutano huo wa bunge, Dkt. Kigwangallah alivitaka vyombo vya usalama ikiwemo polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufanya uchunguzi wa tuhuma hizo.

“Uchunguzi unaendelea, tunakamilisha vielelezo vikikamilika hatua nyingine zitafuata, lakini ninahakikisha tunafanya hivyo, siwezi kusema sana wala kulizungumzia kiundani zaaidi kwa sababu za kiupelelezi,”amesema Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Valentino Mlowola.

Hata hivyo, Dkt. Kigwangalla alizitaja tuhuma zinazomkabili Nyalandu kuwa ni pamoja na ile ya kukodisha chumba kwenye hoteli ya Serena iliyogharimu kiasi cha shilingi bilioni 16 lakini hakusaini mapendekezo mpaka alipotoka madarakani, kashfa ya pili iliyotajwa na waziri huyo ni ile ya kugawa vitalu zaidi ya vitano kwa kampuni za Mwiba Holdings, Wingetwindlos na Tanzania Game Trackers Safari zinazomilikiwa na bilionea kutoka Marekani, huku kashfa ya tatu ikiwa ni ile ya kutumia Helkopta ya kukodi wakati wa kuwania kugombea nafasi ya Urais.

Mugabe akutanishwa na hasimu wake aliyemtimua
Video: Madudu ya Nyalandu yatua Takukuru, Mnyukano mkali lala salama ya kampeni