Mkuu wa mkoa wa Njombe Christopher Ole Sendeka ameagiza kukamatwa na kuwekwa ndani kwa wadaiwa sugu  115 walioshindwa kulipa zaidi ya milioni 300 fedha za benki ya wananchi Njombe NJOCOBA.

Katika kikosi kazi alichokiunda mkuu wa mkoa kusimamia ukusanyaji wa madeni hayo kimefanikiwa kukusanya zaidi ya milioni mia nane hadi sasa huku zikisalia zaidi ya shilingi milioni miatatu.

Bank ya wananchi Njombe ni moja kati ya benki iliyo chini ya ufilisi wa benki kuu ya Tanzania baada ya kushindwa kujiendesha.

Walioshiriki kwa namna moja ama nyingine kuifanya benki ya wananchi Njombe kushindwa kujiendesha wanatajwa kuwa ni pamoja na wadaiwa sugu zaidi ya 300 ambao kati yao wadaiwa 115 waliokopa zaidi ya milioni 300 wameshindwa kurejesha fedha hizo hadi sasa.

“hawastahili kwenda kula pilau,wali,nyama kwa fedha ambazo sio zao”amesema Ole Sendeka

Maamuzi ya mkuu wa mkoa huo Christopher Ole Sendeka ni kukamatwa na kuwekwa ndani ikiwa ni pamoja na kufunguliwa kesi ya uhujumu uchumi, wadaiwa wote walioshindwa kuzirejesha fedha hizo katika kipindi ambacho aliwapa kuzirejesha kwa hiari.

“Niagize kikosi kazi wawakamate na wawekwe ndani na kwamba mtu atatoka mahabusu mara baada ya kumaliza deni lake alilokuwa amelichukua, wadaiwa watakao shindwa kulipa madeni yao ndani ya muda uliowekwa wafikishwe mahakamani wafunguliwe kesi ya uhujumu uchumi na utakatishaji wa fedha kwa kujichukulia fedha za wananchi wanyonge ambazo hawakustahili kuwa nazo” amesema Ole Sendeka

Katika  hatua nyingine Mkuu wa Mkoa amempa muda wa wiki mbili tu mrajisi wa vyama vya ushirika mkoa kuhakikisha anakaa na wadaiwa wote waliokopa fedha katika vyama vya ushirika na saccos ili kumaliza mgogoro uliopo na kurejesha fedha za wananchi ambazo hadi sasa bado zipo mikononi mwao.

Jumla ya Fedha zote zinazo daiwa katika vyama  vya ushirika Saccos pamoja na benki ya wananchi ni zaidi ya bilioni 8.

Tanzania, Kenya zaahidi kuendeleza na kukuza maendeleo
Mdee ashinda kwa kishindo Uenyekiti Bawacha