Polisi nchini Israel wamesema kuwa wamepata ushahidi wa kutosha wa mashtaka ya rushwa na udanganyifu wa fedha dhidi ya Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu na mke wake.

Inadaiwa kuwa Netanyahu na kampuni ya Bezeq telecom walifanya makubaliano yanye thamani ya mamilioni ya dola ili shirika la habari la Walla ambalo ni kampuni ndogo ya Bezeq liwe linachukua mtazamo chanya wakati linaporipoti taarifa zinazomhusu Netanyahu.

Aidha, Netanyahu amekanusha madai dhidi yake, na iwapo atafunguliwa mashitaka, waziri huyo mkuu wa Israel anayetumikia muhula wa nne madarakani atakabiliwa na mojawapo ya changamoto kubwa zaidi kisiasa.

Uamuzi wa mwisho wa iwapo Netanyahu atafunguliwa mashitaka au la utachukuliwa na mwanasheria mkuu wa Israel ambaye bado anatafakari iwapo amshitaki kiongozi huyo na kesi nyingine mbili zinazomkabili za madai ya hapo awali ya rushwa, udanganyifu na uvunjaji wa uaminifu.

Hata hivyo, wachambuzi kadhaa wamesema kuwa huenda, Netanyahu akaitisha uchaguzi mapema zaidi iwapo mashitaka yatafunguliwa dhidi yake. Uchaguzi ujao Israel unatarajiwa mwezi Novemba 2019, lakini huenda kiongozi huyo wa Israel akawania tena na hivyo kumlazimu mwendesha mashitaka mkuu kutafakari upya kabla ya kumfungulia mashitaka.

Video: Membe na Dkt. Bashiru ngoma bado nzito, Magufuli amtaja Lowassa shida ya maji Monduli
Meya wa jiji Dar akamatwa, Polisi wadai alitaka kupora sifa