Jeshi la polisi nchini Misri limesema kuwa limeua wapiganaji 40 wa makundi ya kigaidi waliokuwa wanapanga mashambulizi.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Mambo ya Ndani, polisi waliwavamia magaidi hao katika maficho yao yaliyokuwa Giza na Sinai Kaskazini, jana alfajiri.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa magaidi hao walikuwa wamepanga kushambulia makanisa, askari pamoja na maeneo yenye watalii wengi.

Juzi, wapiganaji wa makundi ya kigaidi walitekeleza shambulizi la bomu katika eneo la Giza kwenye basi la watalii. Hakuna kundi lolote lililojitokeza kudai kutekeleza tukio hilo ambalo lilisababisha vifo vya watalii kutoka Vietnam pamoja na waongozaji wa watalii hao.

Imeelezwa kuwa polisi waliwaua watu 30 katika mashambulizi mawili ya kushtukiza kwenye eneo la Giza, na wengine 10 waliuawa katika eneo la El-Arish ambao ni makao makuu ya jimbo la Sinai Kaskazini.

“Makundi ya magaidi yalikuwa yanapanga kutekeleza mashambulizi katika maeneo ya makanisa na sehemu ambazo wakristo walikuwa wanaabudia. Pia, walipanga kulenga maeneo ya utalii pamoja maeneo mengine ya kiuchumi,” imeeleza taarifa ya Wizara.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, polisi wamekamata vifaa vya kutengenezea mabomu pamoja na idadi kubwa ya silaha.

Video: Magufuli aibua mkanganyiko mpya, Vigogo walioonja joto la jiwe 2018
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Desemba 30, 2018