Klabu ya Real Madrid imetangazwa kuwa klabu ya soka duniani kote iliyoongoza kwa kuingiza fedha nyingi zaidi kati ya mwaka 2017/2018.

Klabu hiyo ya Hispania yenye rekodi ya kushinda makombe ya misimu mitatu mfululizo ya Ligi ya Mabingwa, imeripotiwa kutengeneza $854.8 milioni katika kipindi hicho, kwa mujibu wa Deloitte Football Money League la mwaka 2019.

Klabu ya Barcelona ambayo sasa inaongoza La Liga imechukua nafasi ya pili katika orodha hiyo ikiwa imeingiza $785.5 milioni, na magwiji wa Uingereza, Manchester United ambao mwaka uliopita waliongoza orodha hiyo wameangukia katika nafasi ya tatu wakiwa wametengeneza $758 milioni.

Hii ni mara ya kumi na mbili katika historia kwa Real Madrid kuongoza katika orodha hiyo lakini ni mara ya kwanza tangu msimu wa mwaka 2014/15.

Kwa mujibu wa uchambuzi wa Deloitte, timu 20 za juu kwenye orodha hiyo zilikuwa na ukuaji wa mapato yao kwa ujumla kwa 6%. Walioshika nafasi tatu za juu zaidi yaani Real Madrid, Barcelona na Manchester United kwa pamoja waliingiza $2.3 bilioni ikiwa ni zaidi ya mara mbili zaidi ya mapato yao ya miaka kumi iliyopita.

Jana, mashabiki wa Real Madrid wameipokea habari hiyo kwa furaha iliyosindikizwa na ushindi wa 4-2 dhidi ya Girona.

Nairobi: Al-Shabaab wadaiwa kufungua vibanda 52 vya Simu-Pesa
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Januari 25, 2019