Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ngazi ya Makatibu Wakuu wamekutana na kujadili rasimu ya mpango mkakati elekezi mpya wa maendeleo wa kanda (2020 – 2030) pamoja na rasimu ya dira ya SADC (2020 – 2050) kwa njia ya (Video Conference) jijini Dar es Salaam.

Akiongea mara baada ya kumalizika kwa mkutano huo, Mwenyekiti wa mkutano ambae ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na UShirikiano wa Afrika Mashariki, Brigedia Jenerali, Balozi Wilbert Ibuge amesema kuwa lengo la mkutano huo lilikuwa ni kuangalia mambo mawili makubwa ambayo ni dhima ya SADC kuanzia sasa 2020 hadi 2050 pamoja na mpango mkakati wa SADC kuanzia mwaka 2020 – 2030 kwa sababu mpango mkakati wa SADC uliokuwa unatumika tangu mwaka 1992 umeisha muda wake.   

“Nyaraka hizi mbili ni za muhimu sana kwa sababu hadi sasa hivi toka SADC ilipoanzishwa 1992 imefanya mambo makubwa lakini sasa ule mpango mkakati wake uliokuwa unatumika tangu mwaka 2010 na ambao ulihuishwa mwaka 2015 ukafika hadi 2020 umeisha muda wake hivyo ilikuwa ni muhimu kuandaa rasimu ya nyaraka hizi muhimu,” Amesema Balozi Ibuge.

Ameongeza kuwa, rasimu za nyaraka hizo mbili zitawasilishwa kwenye mkutano wa 40 wa Wakuu wa nchi wanachama wa SADC na Serikali unaotegemewa kufanyika tarehe 17 Mwezi Agosti 2020 kwa njia ya mtandao.

Mpango Mkakati wa SADC ni mpango wa maendeleo ya kanda uliopitishwa na Mkutano wa wakuu wa nchi na serikali wa SADC uliofanyika mwaka 2003 jijini Dar es Salaam na ulianza kutekelezwa rasmi mwaka 2005 kwa kipindi cha miaka 15 (2005  – 2020). Aidha, mpango huo una vipaombele vinne ambavyo ni maendeleo ya viwanda na mtangamano wa soko, miundombinu bora, amani na usalama, pamoja na programu maalum.

“Dira ya SADC 2020 – 2050 inatoa taswira ya Jumuiya kwa miaka 30 ijayo ambapo msingi wake ni amani, ulinzi, utulivu na utawala bora, uchumi wa kati unaoendeshwa na sekta ya viwanda na wanajumuiya wenye hali bora ya maisha,” Amesema Balozi Ibuge.

Hivyo dira ya SADC 2050 ni muhimu kwa maendeleo ya Ukanda wa Kusini mwa Afrika hususan katika kutekeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Dunia 2030 na ajenda ya Umoja wa Afrika ya Mwaka 2063. 

Katika tukio jingine, Brigedia Jenerali, Balozi Wilbert Ibuge amekutana na kufanya amekutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR) nchini Tanzania, Bw. Antonio Canhandula katika ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Balozi Wilbert Ibuge amesema kuwa UNHCR imekuwa na mchango mkubwa sana unaohusisha kulinda haki za wakimbizi lakini pia kuwarejesha wakimbizi nchini mwao.

Pamoja na mambo mengine, mazungumzo yalilenga kuimarisha uhusiano baina ya Tanzania na Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR) kwa ujumla.

Lissu kuchukua fomu ya urais leo

NCCR-Mageuzi urais Zanzibar yatoka kapa

Ndege yenye abiria 190 yaanguka uwanja wa ndege India
Lissu kuchukua fomu ya urais leo