Serikali kupitia Taasisi ya Saratani ya Ocean Road imenunua mashine mbili mpya za kisasa zenye thamani ya shilingi bilioni 9.56 kwa ajili ya kutoa tiba ya mionzi kwa wagonjwa wa Saratani hapa nchini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu wakati akizungumza kuhusu utekelezaji wa wizara hiyo.

“Mashine hizi za kisasa zimeboresha utoaji wa tiba ya mionzi hasa kupunguza muda wa kutoka wiki 6 hadi wiki 2 kwa mgonjwa mpya wa Saratani ambaye anapaswa kuanza tiba hiyo,” amesema Ummy.

Aidha amesema kuwa hali ya upatikanaji wa dawa kwa wagonjwa wa Saratani katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road imeimarika kutoka asilimia 4 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 85 mwezi Julai mwaka huu.

Katika hatua nyingine, amesema kuwa Serikali imeboresha huduma za hospitali za rufaa za kanda kwa kufungua majengo mapya na kufunga mashine za mionzi ya tiba ya Saratani katika hospitali za KCMC mjini Moshi, Bugando Jijini Mwanza na Hospitali ya Rufaa ya Mbeya hatua ambayo itasaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road.

Hata hivyo, ameongeza kuwa hali ya upatikanaji wa dawa muhimu kwa ujumla katika maeneo yote hapa nchini umeimarika hadi kufikia asilimia 89.6 kutoka asilimia 35 mwaka 2015.

 

Watano kizimbani kwa jaribio la kumuua Waziri Mkuu
Maoni hasi kazini: Namna ya kukabiliana nayo kwa ufanisi