Mabingwa wa soka Tanzania Bara na Kombe la Shirikisho (ASFC), Simba SC wanahusishwa na taarifa za kuwasajili wachezaji wa kimataifa Jesse Were wa Zesco United na beki wa klabu ya Chippa United ya Afrika Kusini, Frederic Nsabiyumva.

Were ambaye ni mchezaji wa timu ya taifa ya Kenya, aliwahi kuzichezea Mathare United na Tusker za nchini humo kabla ya kujiunga na Zesco ya Zambia.

Pia, Nsabiyumva ni mchezaji wa timu ya taifa ya Burundi aliyewahi kuichezea Atletico Olimpic Bujumbura, akajiunga na Jomo Cosmos na mwaka juzi na baadae kusajiliwa na Chipa United zote za Afrika kusini.

Licha ya klabu hiyo kutoweka wazi juu ya usajili huo, Mtendaji wa klabu hiyo Senzo Mazingisa, hivi karibuni alisema wanatarajia kufanya maboresho ingawa wanapata wakati mgumu wa kuamua nani wa kumuacha ili kufanya ingizo jipya.

Alisema watasajili kulingana na ripoti watakayopewa na kocha Sven Vandebroeck kujiandaa na michuano ya kimataifa msimu ujao wa 2020/21.

Kwa upande wa Young Africans, licha ya kusajili wachezaji watano wazawa, bado wanatajwa huenda wakati wowote wakamtangaza Salum Abubakari kutoka Azam FC na Farid Mussa kutoka Tenerife ya Hispania na baadaye watahamia kimataifa.

Wachezaji iliowasajili mpaka sasa ni Waziri Junior kutoka Mbao, Yassin Mustapha kutoka Polisi Tanzania, Bakari Mwamnyeto kutoka Coastal Union, Zawadi Mauya kutoka Kagera Sugar na Abdallah Shaib (Ninja) .

Kwa upande wa Azam FC, imewasajili Ally Niyonzima kutoka Rayon Sport ya Rwanda, Ismail Aziz kutoka Tanzania Prisons, Awesu Awesu kutoka Kagera Sugar, Ayoub Lyanga kutoka Coastal Union na David Mapigano Kissu kutoka Gor Mahia ya Kenya.

Namungo FC wakwama usajili wa Ajibu, Mobby
Habari kubwa kwenye magazeti leo, Agosti 7, 2020