Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesema katika kipindi cha muhula wa pili wa miaka mitano ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli itajikita zaidi katika diplomasia ya uchumi, kuimarisha sekta binafsi, kukuza biashara pamoja na mahusiano na Mataifa mengine duniani.

Msimamo wa Tanzania umetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi Jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano wake na Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao hapa Tanzania pamoja na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa.

“Katika mwaka huu unaoanza sasa na miaka ijayo katika muhula wa pili awamu ya tano ni wakati muafaka wa Tanzania kuimarisha diplomasia ya uchumi na uhusiano mwema baina yake na nchi mbalimbali kwa kuwakaribisha wawekezaji kutoka nchi hizo katika maeneno ya uzalishaji, viwanda na kuongeza biashara kwa manufaa ya mataifa yote,” amesema Prof. Kabudi.

Aisha Prof. Kabudi ameueleza Mkutano huo kuwa hali ya kisiasa na amani Zanzibar na Tanzania kwa ujumla imeimarika kuliko wakati wowote hususani mara baada ya uchaguzi mkuu uliomalizika Octoba, 2020 na kwamba uwepo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar unachochea kuongezeka kwa uwekezaji na ufanyaji wa biashara kwa lengo la kukuza uchumi.

Kwa upande wake Kiongozi wa Mabalozi Dkt. Ahmada El Badasui ambaye pia ni Balozi wa Comoro nchini ameshukuru kwa uwepo wa mkutano huo ambao unawapa fursa mabalozi kufahamu masuala mbalimbali yanayoendelea hapa nchini.

“Nakupongeza Mhe. Waziri na uongozi wa Wizara kwa kuandaa mkutano huu ambao unatupa fursa sisi mabalozi kujadili na kujua mambo mbalimbali yanayoendelea hapa nchini, mikutano kama hii ni muhimu sana kwetu kwani inatusaidia na kutuwezesha kuboresha mahusiano yetu ya kidiplomasia,” amesema Dkt. El Badasui.

Kwa upande wake Balozi wa Umoja wa Ulaya Manfredo Fanti ameipongeza Tanzania kwa kuingia uchumi wa kati na kwamba Umoja wa Ulaya uko tayari kutoa ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha Uchumi wa Tanzania unaendelea kukua na kuimarika.

Mkutano huo wa Mabalozi na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa umehudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki William Tate Ole Nasha, Katibu Mkuu Balozi, Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge na Wakurugenzi na Wakuu wa Idara na vitengo vya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Tanzania kung'aa utekelezaji wa miradi Afrika
Habari kubwa kwenye magazeti leo, Februari 6, 2021