Yasimwayo kuhusu uwepo wa uhusiano wa kimapenzi kati ya rapa Drake na Kim Kardashian, ambayo yalitokana na wimbo wa ‘In My Feelings’ wa rapa huyo yamepashwa moto na kuteka vichwa vya habari kivingine.

Awali, Nick Cannon ndiye aliyefungua pazia la tetesi hizo za uhusiano kati ya Kim K ambaye ni mke wa Kanye West na Drake ambaye awali alikuwa rafiki wa Kanye kabla ya wawili hao kuingia kwenye mkwaruzano. Cannon alidai kuwa ‘Kiki’ anayeimbwa kwenye ‘In My Feelings’ ni Kim Kardashian, hali iliyochochewa pia na bidhaa za urembo za Kim K kubatizwa jina la ‘Kiki’.

Cannon akiwa kwenye ‘Everyday Struggle’, alizua jambo akidai kuwa kuna sababu kwanini Kanye West aliamua kuvujisha siri za Drake kwa Pushat T ambaye alimmaliza kwenye wimbo wake alipoziweka hadharani.

Alidai kuwa sababu ni Kanye aliogopa kuwa huenda Drake asingepunguzwa nguvu angekuja kutoa siri hiyo ya kuwa na uhusiano na mkewe.

Hata hivyo, watu wa karibu wa Kim Kardashian wamejitokeza na kujibu tuhuma hizo kwa niaba yake, wakidai kuwa mrembo huyo mwenye watoto watatu hakuwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi kwa namna yoyote na Drake katika historia yake.

Kwa mujibu wa watu hao, jina la ‘Kiki’ la bidhaa za Kim Kardashian na jina hilo la mrembo ambaye ameimbwa na Drake ni vitu viwili tofauti na kwamba imetokea kufanana kwa bahati tu.

Wakati watu hao wa karibu wakifunguka kupitia vyombo vya habari wakimtetea Kim K, mrembo huyo yeye anaonekana kuendelea na maisha yake kama vile hakuna kilichozungumzwa.

Wakati huohuo, Drake ambaye mauzo ya albam yake ya ‘Scorpion’ yalikuwa jibu la mwiba kwa mahasimu wake Pusha T na Kanye West, aliwahi kuonekana tena akiwa jukwaani ambapo alimchana Kanye kiaina.

Hivi karibuni, Kanye alijitokeza kukanusha tetesi kuwa yeye ndiye aliyevujisha siri za Drake kwa Pusha T na kumuomba radhi rapa huyo kwa usumbufu uliojitokeza.

Bosi huyo wa Good Music ameendelea kujieleza kuwa amebadilika na kwamba ni mtu mpya na achukuliwe hivyo.

Video: Dkt. Kamani atoa onyo kali kwa viongozi wa vyama vya ushirika
LIVE: Rais Magufuli akihutubia wananchi wilayani Serengeti mkoa wa Mara