Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa utabiri wa mwelekeo wa mvua za vuli, kuanzia mwezi Oktoba hadi Disemba, 2019.

Akizungumza katika mkutano na wanahabari, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes L. Kijazi amesema mifumo ya hali ya hewa ilivyo kwasasa na jinsi inavyotarajiwa kuwa kwa kipindi cha Oktoba hadi Disemba, 2019 – mvua za wastani hadi chini ya wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya Nyanda za juu kaskazini mashariki pamoja na Pwani ya kaskazini.

Amesema kuwa ukanda wa Ziwa Viktoria pamoja na maeneo ya kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma (Kibondo) yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani, huku maeneo mengi ya nyanda za juu kaskazini mashariki pamoja na pwani ya kaskazini yakitarajiwa kuwa na mvua za wastani hadi chini ya wastani.

Amebainisha kuwa mvua za wastani hadi juu ya wastani zinatarajiwa katika maeneo ya ukanda wa Ziwa Viktoria pamoja na kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma. Kanda ya Ziwa Viktoria mikoa ya Kagera, Mara, Mwanza, Geita, Simiyu na Shinyanga.

“Maeneo machache ya mkoa wa Kagera mvua za nje ya simu zinaendelea toka mwezi Agosti na zinatarajiwa kusambaa katika maeneo mengine ya ziwa Viktoria hadi kufikia wiki ya pili ya mwezi Oktoba, hivyo kuungana na msimu wa mvua za Vuli,”amesema Dkt. Kijazi

Aidha, amebainisha kuwa msimu wa mvua za vuli katika maeneo haya unatarajiwa kuisha kati ya wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi Januari, 2020. ambapo amesema kuwa kwa Mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, mvua zinatarajiwa kuanza katika wiki ya pili ya mwezi Oktoba ingawa mtawanyiko wake unatarajiwa kuwa hafifu.

Kwa upande wa Nyanda za juu Kaskazini Mashariki katika Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara, zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Oktoba na zinatarajiwa kuwa za wastani hadi chini ya wastani katika maeneo mengi ya mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara. Mvua hizo zinatarajiwa kuisha katika wiki ya nne ya mwezi Disemba 2019.

Kwa upande wa tahadhari, TMA imesema kuwa katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani, upungufu wa unyevu nyevu ardhini unatarajiwa kujitokeza pamoja na upungufu wa malisho na maji kwa ajili ya mifugo hivyo kuna uwezekano wa kusababisha migogoro kati ya wakulima na wafugaji.

LIVE Bungeni Jijini Dodoma leo Septemba 4, 2019
RC Makonda awasilisha muswada wa marekebisho ya sheria ya mirathi