Katibu wa Mwenezi wa Chama cha ACT- Wazalendo, Ado Shaibu amesema kuwa kama Mbunge wa Siha kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Godwin Mollel kuwa akithibitisha madai yake kuwa 1.5 Trilioni ambazo wapinzani wanadai matumizi yake hayajulikani kwamba ni makusanyo ya Zanzibar ambayo yalirekodiwa katika vitabu vya TRA, basi yeye atahama ACT Wazalendo na kujiunga na CCM.

Ado ameandika hayo kupitia ukurasa wake wa ‘Twitter’ wakati akijibizana na Dkt. Mollel, ambapo Shaibu alidai kuwa hana mpango wa kuhamia CCM lakini alimjibu vile Mollel kwakuwa alijua hana uwezo wa kuthibitisha.

“Sina mpango wa kuhamia CCM. Nimempa changamoto Dkt. Mollel kwa sababu najua hana ubavu wa kuthibitisha hilo. amekurupuka tu ili apate kiki kupitia Zitto ili na yeye apate kusikika, angekuwa msomi kweli angekwenda kutazama mapato ya Zanzibar kwa mwaka husika kisha angejua anachoongea hakipo,” amesema Ado.

Aidha, katika mjadala huo, Ado amesema kuwa yeye sio mhasibu na wala hakuwepo kwenye kikao cha kamati ya PAC. lakini akasema kuwa kama Dkt. Mollel akimthibitishia kwamba CAG kasema fedha yote 1.5T ni hela ya Zanzibar iliyoonekana kwenye mahesabu ya TRA basi atajiuzulu nafasi yake ya katibu uenezi wa ACT-Wazalendo na kujiunga na CCM. 

Hata hivyo, mjadala huo ulizuka mara baada ya Dkt. Mollel kuonekana kumshambulia Zitto Kabwe ambaye ni kiongozi wa chama cha ACT-Wazalendo na Mbunge wa Kigoma mjini, kupitia mtandao wake wa Twitter aliporipoti hoja ya 1.5 Trilioni kupelekwa rasmi kwenye kamati ya PAC.

Katika ukurasa wake wa Twitter, Dkt. Mollel ameandika kuwa ”Mh zitto Natumai sasa utaacha kimbelembele, CAG kakuumbua kuwa ulikuwa unasema uongo, amekuonyesha kuwa 1.5T ni fedha iliokusanywa Zanzibar na inatumika Zanzibar na haijaja bara ila imeonyeshwa tu kwenye ripoti za TRA,” ameandika Dk. Mollel.

 

DC Msafiri awacharukia watumishi Njombe
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Januari 26, 2019