Na Allawi Kaboyo, Karagwe.

Wakati Tanzania ikiwa katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu wa madiwani,wabunge na rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania, mgombea urais kupitia Chama cha wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, amesema uchaguzi huu usiwe chanzo cha uvunjifu wa amani ya Tanzania.

Lipumba ametoa kauli hiyo leo Septemba 24, kwenye mkutano wake wa hadhara wa kuomba kura katika uwanja wa Changarawe uliopo mjini Kayanga wilaya ya Karagwe mkoani Kagera, ambapo amesema Tanzania imekuwa kisiwa cha amani kwa kipindi kirefu hivyo watanzania wanao wajibu wa kuhakikisha amani hiyo inadumu hasa katika kipindi hiki cha uchaguzi.

Amesema kuwa vyama vya siasa vinatakiwa kuwa mfano wa kuigwa katika kuhubiri amani huku akiomba tume ya uchaguzi nchini kuhakikisha inasimamia uchaguzi huu kuwa wa huru na haki suala litakalopelekea nchi kudumu katika amani kwa kuwa haki itatendeka.

“Amani hii tuliyonayo tunapaswa kuilinda na kuhakikisha inadumu, niiombe tume yetu ya uchaguzi ihakikishe uchaguzi huu unakuwa wa huru na haki na ikifanya hivyo hakika amani yetu itastawi katika misingi ya tuliyoasisiwa, CUF tunaamini katika amani na sera yetu imejikita katika haki sawa kwa wote” Amesisitiza Prof. Lipumba.

Ameongeza kuwa anatambua pia wananchi wa wilaya ya Karagwe wanazo changamoto nyingi ikiwemo kero sugu ya maji pamoja na migogoro ya ardhi inayowapelekea wengi wao kupoteza haki na hivyo kuwaomba wanankaragwe kumchagua ili kuweza kuwasaidia kutatua kero hizo kwa muda mfupi.

Kwa upande wake, mgombea udiwani kata ya Kihanga wilayani humo kupitia chama hicho Anastella Kibake, amemuomba mwenyekiti wake na mgombea urais endapo atapewa ridhaa na watanzania kuiongoza nchi hii kuwasaidia wakina mama wajane na watoto yatima wasidhulumiwe haki zao.

Anastella ameongeza kuwa wananchi wa kata hiyo wanakabiliwa na changamoto ya huduma za afya hasa wakina mama wajawazito kwa kutozwa fedha nyingi wanapokwenda kujifungua hali inayowapelekea wanawake hao kuhatarisha maisha yao pamoja na watoto wao kwakuwa wamekuwa wakijifungulia majumbani kwa kuogopa gharama.

Nje ya kero hizo amesema kuwa wanawake wamekuwa wakitaabika kwa kutembea mwendo mrefu kufata huduma ya maji ambapo wamekuwa wakishindwa kufanya shughuli nyingine za kuwaongezea kipato na wengine kuhatarisha ndoa zao.

Akijibu hoja hizo Prof.Lipumba kwanza amewaomba wananchi wa Kihanga kumchagua diwani huyo kwakuwa anayo maono na hasa matatizo yanayowakumba kina mama na yeye atahakikisha anamsaidia.

Lipumba amesema katika kipindi chake cha uongozi endapo atachaguliwa huduma za afya zitakuwa karibu na wananchi na kuwa rafiki lakini pia kuweka ufumbuzi wa kudumu katika kuhakikisha wananchi wananufaika na mema ya nchi.

Serikali yamjibu Lissu
Mauaji ya Breonna Taylor: Taharuki yatanda Marekani