Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Rex Tillerson amekutana na Waziri mwenzake wa Mambo ya Nje wa Urusi, Sergei Lavrov kwaajili ya kujadili mzozo wa Syria ambao umesababisha vifo vya watu wasiokuwa na hatia na wengine kuikimbia nchi hiyo kufuatia machafuko ya kisiasa.

Tillerson na Lavrov wamekutana mjini New York, kabla ya kuanza kwa mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, na wamekubaliana kujiepusha na mapambano ya kijeshi nchini Syria ili kupunguza ghasia na kuanzisha masharti ili mchakato wa Geneva uweze kusonga mbele.

Aidha, baada ya mkutano wa mawaziri hao, uliofanyika kwenye ubalozi wa Urusi katika Umoja wa Mataifa, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Tillerson aliondoka bila ya kuzungumza chochote na waandishi habari, ambao awali walialikwa kuhudhuria mazungumzo hayo.

Hata hivyo, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Urusi, Maria Zakharova, amesema kuwa mkutano huo ulihusu ushirikiano katika mzozo wa Syria, masuala ya Mashariki ya Kati na makubaliano ya Minsk.

Ferdinand kuingia katika masumbwi
Israel na Marekani zaunda kambi ya pamoja ya jeshi la anga