Wanakijiji zaidi ya 200 wa Kijiji cha Kishanda B Wilaya ya Kyerwa Mkoani Kagera, wamevamia shamba la mwananchi mwenzao kisha kuikatakata migomba yote, kuchinja mifugo huku mbuzi wengine wakiwaua kwa kuwachoma na moto.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Ahmed Msengi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza vitu vilivyoharibiwa ni pamoja na mashamba ya Migomba, Kahawa na Miti pamoja na kuwaua Mbuzi wanne na kuwajeruhi mbuzi wawili, huku chanzo cha mgogoro huo ni umiliki wa ardhi kubwa, mgogoro ambao tayari ulishafika mahakamani.

Aidha, tukio hilo lilifanywa wakati mwenye shamba na mifugo iliyoharibiwa, Tryphone  Jeremiah akiwa katika ibada kanisani na kudai kwamba wananchi hao takribani 200, walivamia mashamba na mifugo hiyo saa 6:00 mchana, baada ya kuwepo mgogoro wa ardhi baina ya baba yake na wanakijiji hao tangu mwaka 2007.

“Wananchi wanalalamika kuwa ninamiliki ardhi kubwa, baada ya wanakijiji hao kuvamia mashamba kwa makundi makundi, waliyafyeka kwa muda fupi na kuua mbuzi na kuwachoma moto pamoja na kubomoa nyumba,” amesema Jeremiah.

Inaelezwa kuwa wananchi hao walitumia takribani masaa matatu kutekeleza unyama huo na kwa mujibu wa mlalamikaji (Jeremiah), anasema alikuwa na mbuzi 100, hivyo kati ya wale waliochinjwa na waliobaki hai wanaonekana 39 na mbuzi 57 hawajulikani walipo.

Pinda aigeukia CRDB, ‘tuelekeze nguvu zetu huku’
Lugola aitaka bodi ya Magereza kuhakikisha inajitosheleza kwa chakula