Jimbo la Alabama nchini Marekani limepitisha muswada wa sheria inayowalazimu baadhi ya watu waliopatikana na hatia ya kuwabaka watoto, waondolewe nguvu za kiume kupitia njia ya kemikali.

Chini ya sheria hiyo, wale watakaobainika kuwa na hatia ya kosa la kuwabaka watoto wenye umri chini ya miaka 13 watalazimika kuanza kupata dawa za kuwapunguzia uwezo wa kufanya tendo la ndoa huku wenye hatia watatakiwa kulipia matibabu kabla ya kuachiliwa kwa msamaha.

Hadi sasa kuna majimbo saba , yakiwemo Louisiana na Florida, yenye sheria ya kuwaondolea nguvu za kiume kwa wale wote wanaopatikana na hatia ya kuwabaka watoto wadogo.

Aidha, Muswada wa sheria hiyo ulitiwa saini na Gavana wa jimbo la Alabama nchini humo, Kay Ivey Jumatatu, huku akisema hii itakuwa ni hatua nzuri ya kuelekea kuwalinda watoto katika jimbo la Alabama.

Hatua hiyo awali ilipendekezwa na Mbunge wa chama cha Republican, Steve Hurst ambapo alisema kuwa amekuwa akiathirika sana kwa kusikia matukio mbalimbali na kusikiliza ushahidi kutoka kwa mashirika yanayowalea watoto kuhusu namna watoto wadogo wanavyobakwa.

Hata hivyo, Muswada huo umekosolewa vikali na Muungano wa mashirika yanayopigania uhuru wa raia katika jimbo la Alabama, huku Mkurugenzi Mkuu wa Muungano huo, Randall Marshall akisema haijawa wazi kwamba ni kweli zina athari yoyote na ikiwa imethibitishwa kimatibabu.

 

 

Trump adai yuko tayari kufanya mazungumzo na Kim Jong Un
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Juni 12, 2019