Makamu  wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu  Hassan ametoa wito kwa Bodi ya wahandisi nchini (ERB) kupitia Kitengo cha wahandisi wanawake kuandaa kampeni mbalimbali zitakazohamasisha na  kuhimiza wanafunzi wakike  kusoma masomo ya sayansi.
Wito  huo umetolewa leo jijini Dare es Salaam wakati wa uzinduzi wa kongamano na maonyesho ya wanawake wahandisi lililoandaliwa na Bodi hiyo.
Makamu huyo amesema kuwa lengo la kampeni hizo ni kushawishi wanafunzi wakike kupitia mashuleni ili kuwahimiza wanafunzi hao kujiunga na fani ya uhandisi.
“Udahili wa wanawake wanaosoma masomo ya Sayansi umebaki kuwa wa chini hivyo waongeze ushawishi kwa wasichana katika kusoma masomo ya sayansi hii itapelekea kuongeza idadi ya wanawake wahandisi  nchini,” Aliongeza Mhe Samia.
 Aidha, alisema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa wahandisi katika maendeleo ya nchi hususani katika sekta za Nishati, Madini, barabara, maji, na kilimo huku ikiendelea kuweka mipango madhubuti ya kuinua na kuimarisha fani ya uhandisi.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya ambaye alikuwa Rais na Mwenyekiti wa Kitengo cha wahandisi wanawake katika Bodi ya wahandisi nchini amesema kuwa Wizara imejipanga kuhakikisha kwamba masomo ya sayansi yanapewa kipaumbele ili kuhakikisha wanawake wanafikia malengo ya viwanda na uchumi wa kati 2025 kwakuwa wao ndio wahamasishaji wa mabadiliko.
“Sayansi inaanzia vijijini tatizo ni miundombinu hafifu jambo linalofanya wasichana wengi wasifikiwe, hivyo natoa ombi kusaidia  maabara zilizoanzishwa vijijini ili ziwe bora na hivyo  kuwawezesha wanafunzi hasa wanasichana kuwa na mazingira mazuri” aliongeza Mhandisi Manyanya.
Naye Msajili wa Bodi ya wahandisi nchini(ERB) Mhandisi Steven Mlote amesema kuwa uwiano kati ya wahandisi wanawake na wahandisi wanaume umeongezeka kutoka 1 kwa 27 hadi 1 kwa 14 hivyo kushauri wanawake kupewa nafasi mbalimbali za uongozi.
Mwakilishi kutoka Ubalozi wa Norway nchini amesema kuwa Serikali yao inawasaidia wanawake wahandisi ili kuwawezesha na  kunufaisha taifa kiuchumi na kijamii.
Serikali ya Norway imetoa jumla ya Shilingi Bilioni 4.3 za kitanzania kuchangia mpango wa miaka miaka mitano (2016-2021) ambao utasaidia kuwajengea uzoefu wahandisi wanawake 150.

Mpinga Cup Yazinduliwa Wilaya Ya Ilala
Sekta Za Maendeleo Zaombwa Kuwekeza Dodoma