Rais wa Uganda, Yoweri Museveni aambaye amekuwa madarakani katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki tangu 1986, ametia saini kupitisha sheria inayoharamisha baadhi ya shughuli za mtandao, licha ya wasiwasi kuwa sheria hiyo inaweza kutumika kunyamazisha ukosoaji halali wa mtu moja mmoja na vyombo vya Habari.

Mswada huo, uliopitishwa na Bunge Septemba 2022, na uliletwa na mbunge ambaye alisema ni muhimu kuwaadhibu wale wanaojificha nyuma ya kompyuta ili kuumiza wengine akisema “kufurahia haki ya faragha kunaathiriwa na matumizi mabaya ya majukwaa ya mtandaoni na mitandao ya kijamii kwa kushiriki habari zisizoombwa, za uongo, chuki, chuki na zisizostahiliwa.”

Sheria hiyo mpya, inatajwa kuongeza vikwazo katika sheria yenye utata ya 2011 kuhusu matumizi mabaya ya kompyuta ambapo pia inapendekeza kifungo cha hadi miaka 10 katika visa vingine, ikijumuisha kwa makosa yanayohusiana na uwasilishaji wa habari kuhusu mtu bila ridhaa yake na kushiriki au kuingilia habari bila idhini.

Mgahawa wa Internet nchini Uganda. Picha: africanews

Wapinzani wa sheria hiyo wanasema itaminya uhuru wa kujieleza katika nchi ambayo wapinzani wengi wa Museveni, kwa miaka mingi hawawezi kufanya maandamano mitaani, mara nyingi huibua wasiwasi wao kwenye Twitter na tovuti zingine za mtandaoni huku wakisema hilo ni pigo kwa uhuru wa kiraia mtandaoni.

Kamati ya Kulinda Waandishi wa Habari nchini humo imesema, Wabunge wa Uganda wamechukua mkondo mbaya katika kujaribu kufanya sheria ambayo tayari ina matatizo ili iwe mbaya zaidi na sasa sheria hiyo itafanya mamlaka kutumia nafasi hiyo kuwalenga wachambuzi wakosoaji na kuadhibu vyombo huru vya habari.

Kenya yakanusha madai kutolipa deni la China
Rais atoa angalizo kwa jamii ugonjwa wa Ebola