Wanafunzi wa Kidato cha kwanza waliotoka katika kijiji cha Lilido Halmashauri ya wilaya ya Mtwara wameondokana na usumbufu wa kusafiri hadi kata Jirani ya Libobe kufuata shule ya Sekondari, baada ya kukamilika kwa vyumba vitano vya Madarasa vilivyojengwa kwa michango na nguvu za wananchi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti tofauti na Dar24 Media, wakati wakifanya usafi kwenye shule hiyo Mpya waliyo hamishiwa watoto wao (Shule ya sekondari Kitere) baadhi ya wazazi na walezi wamesema kuwa wamelazimika kujitolea Michango na nguvu kazi kujenga shule hiyo kutokana na usumbufu wanaokumbana nao watoto wao wa kutembea umbali mrefu kufuata shule kata jirani.

“Hapa tulianza kwa kila Kaya kutoa shilingi Elfu therathini, tukaja kutoa tena kidogo kidogo pamoja na kuwekeana zamu za kuja kujitolea nguvu kazi za kusafisha eneo,Kuchimba Msingi, mpaka kusogeza Matofali na kuchanganya Zege mpaka leo unaona majengo haya yote yaliyo simama lakini tumefanya hivi kutokana na usumbufu wa watoto wetu kwenda kusoma kule Libobe wakati Nguvu na maeneo ya kujenga tunayo”.Amesema Bakari Mohamedi ambaye ni mmoja wa wananchi aliyekua akishiriki kufanya usafi.

Kwa upande wake Afisa Elimu Sekondari Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara mkoani humo, Fadhiri Mvungi ambaye alitembelea shule hiyo akiambatana na mkuu wa wilaya hiyo, Evod Mmanda, amesema kuwa kilichofanyika ni kutekelea maagizo ya Naibu waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mwita Waitara ambaye alitembelea shule hiyo mwezi uliopita akiwa katika ziara yake mkoa wa Mtwara na kuagiza shule hiyo isimamiwe na baada ya kukamilika wanafunzi wa kidato cha kwanza wahamishiwe katika shule hiyo.

Naye Mkuu wa wilaya hiyo ya Mtwara, Evod Mmanda, amewapongeza wananchi hao kwa juhudi walizofanya pamoja na mbunge wa jimbo la Mtwara Vijijini, Hawa Ghasia kwa uhamasishaji aliofanya wakati wa ujenzi pamoja na wadau mbalimbali waliojitolea michango yao.

Shule hiyo ya Sekondari ya Kitele ilianzishwa kwa nguvu za wananchi imetembelewa na viongozi mbalimbali akiwemo Mbunge wa jimbo la Mtwara Vijiji, Hawa Ghasia ambaye ndiye aliyeweka jiwe la Msingi Machi, 2018 Pamoja na Naibu waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mwita Waitara, ambapo kwa mujibu wa wananchi hao malengo yao ni kukamilisha ujenzi wa vyumba vilivyo baki kuwawezesha watoto wao kupata Elimu ya sekondari hadi kidato cha Nne kabla ya kuanza mchakato mpywa wa Kujenga madarasa mangine ya Kidato cha Tano na sita.

Wakulima watakiwa kuacha Kilimo cha mazoea
Takukuru yatoa elimu kuhusu Rushwa mkoani Lindi