Wananchi wametahadharishwa kujihusisha na vitendo vya ujangili kwa kudhani kuwa jeshi la polisi limejikita katika kuangazia kampeni za uchaguzi pekee.

Kamanda wa polisi mkoa wa Simiyu, SACP Henry Mwaibambe, ametoa tahadhari hiyo kufuatia uwepo wa watuhumiwa watatu wanaoshikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma za kupatikana na nyara za serikali.

Kwa kushirikiana na askari wa pori la akiba la Maswa jeshi la polisi limefanikiwa kuwakamata Saguda Limbu (20), Saguda Nila (18) na Juma Bayege (21) ambao wamekutwa na nyama ya Pundamilia na Nyumbu zilizo hifadhiwa katika makazi yao.

“Wanyama hawa ni urithi wa taifa, tunaangazia kampeni za uchaguzi lakini haiwezi kuwa ni sababu ya vitendo vya uhalifu, kila mahali tupo na tunafanya kazi,” alisema Mwaibambe.

Aidha, watuhumiwa walikutwa na nyara za serikali ambazo ni vipande vya nyama ya Pundamilia kilo 109, Nyama ya Nyumbu kilo 15.5, pamoja na pikipiki moja ambayo ilikuwa inatumika kusafirishia nyara hizo.

Watuhumiwa hao watafikishwa mahakani siku ya jumatatu kwa makosa ya kujihusisha na ujangili wa wanyapori na kupatikana na nyara za serikali bila kibali.

Zlatko awasili Dar, kusaini miwili Young Africans
Baada ya miezi mitano Shule kufunguliwa tena - Wuhan