Jumla ya wasichana elfu 4000 kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Lindi na Nachingwea Mkoani Lindi wanatarajiwa kufikiwa na Mradi wa lishe kwa watoto wa kike (GIRLS POWERD NUTRITION) unaoendeshwa na World Association of girls guide and girl scouts.
 
Hayo yamesemwa na Meneja wa Mradi huo, David Mbimila wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa usimamizi wa Mradi huo kwa Viongozi wa Girl Guide wa Manispaa ya Lindi, ambapo amesema kuwa Mradi huo wa Lishe kwa watoto wa kike duniani unafanyika kwa majaribio katika nchi tano ikiwemo Tanzania, Bangladesh, Sirilanka, Ufilipino na Madagascar
 
“Kwa Tanzania Mradi huu unatekelezwa katika Mikoa sita ikiwemo Mkoa wa Dar-es-salaam, Tanga, Arusha, Lindi, Dodoma pamoja na Mkoa wa Mara ambapo kwa Mkoa wa Lindi kwa kuanzia tutaanza na Halmashauri ya Manispaa ya Lindi pamoja na Wilaya ya Nachingwea ambapo matarajio yetu ni kuwafikia wasichana elfu nne mpaka ifikapo 2020,”amesema Mbimila
 
Aidha, Mbimila ameyataja malengo ya Mpango huo kuwa ni kutoa Elimu ya Lishe kwa watoto wa kike ili waweze kula vizuri, kukua vizuri, kuongeza nguvu kazi ya kitaifa, huku akiongeza kuwa lengo jingine ni kutaka kuishahuri Serikali kuweka Mada ya Lishe kwa Watoto wa kike katika vikao na mikutano yao wanayoifanya mara kwa mara.
 
Kwa upande wake, kamishina wa Girls Guide Mkoa wa Lindi, Grecy Chipanda amesema kuwa kati ya wasichana hao elfu 4000 watakaonufaika na Mradi huo wasichana 2700 watatoka Halmashauri ya Manispaa ya Lindi huku 1500 watatoka Wilayani Nachingwea.
 
Naye Mwenyekiti wa Girls Guide Mkoa wa Lindi Mwalimu mstaafu, Zuhura Mohamedi amesema kuwa baada ya mradi huo wa Lishe kwa watoto wa kike wa majaribio kumalizika mwaka 2020 matarajio yake ni kuona wasichana Wanashiriki kikamilifu katika masomo yao pasipo kukosa kuhudhuria darasani.
 
Awali akifungua warsha hiyo ya siku nne katibu tawala Mkoa wa Lindi, Dkt. Bora Haule amesema kuwa kama mkoa wamefarijika kuona Mkoa wao ni miongoni mwa Mikoa sita inayotekeleza mradi huo, huku akieleza kwamba Mradi huo utakuwa unaunga mkono jitihada zinazofanywa na mkoa huo za kuongeza ufaulu kwa Watoto wa kike sambamba na kutokomeza mimba za utotoni kupitia kampeni ya “TUMSAIDIE AKUE, ASOME, MIMBA BAADAE”

Katibu wa hamasa na Chipukizi ahamasisha elimu mkoani Njombe
LIVE : Rais Magufuli akifungua kiwanda cha kubangua Korosho Mtwara