Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameziagiza Wizara, Taasisi, Mashirika yote ya Serikali na Sekta Binafsi pamoja na vikundi vya uzalishaji vinavyotumia nishati ya kuni na mkaa zianze kutumia nishati mbadala kwa kupikia na shughuli nyingine za uzalishaji.

Ametoa wito huo leo Juni Mosi, 2021 wakati akitoa tamko kuhusu Wiki ya Mazingira Duniani, katika ukumbi wa Hazina, jijini Dodoma.

Amesema kuwa taasisi kama shule, vyuo, hospitali na majengo makubwa zinapaswa kuzingatia ufungaji wa mifumo ya nishati ya gesi kwa ajili ya kupikia.

“Kila Wizara ifanye ufuatiliaji kwenye taasisi zake na nipatiwe taarifa ya hali ya utekelezaji kila baada ya miezi sita inayoonesha ni taasisi ngapi zimefikiwa, zimebadili mifumo au zimejenga majengo kwa kuzingatia hitaji la nishati mbadala”

“Suala la uhifadhi, utunzaji, usimamizi na usafi wa mazingira lisiwe jambo linalofanyika wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani pekee, bali tujenge tabia ya kuliona kwamba ni suala la kila siku” amesisitiza

Aidha, Waziri Mkuu amewataka viongozi wa Jiji la Dodoma wahakikishe wanaweka mkakati ili maeneo yote yanayopimwa yapandwe miti na kila anayepata kiwanja aelimishwe kuhusu umuhimu wa kupanda miti.

Naye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Selemani Jafo amesema kuwa katika maadhimisho haya watafanya semina kwa maafisa mazingira kutoka TAMISEMI.

“Maafisa mazingira hawa hawakuwa wanatumika vizuri, kupitia maadhimisho haya tutabadilishana mawazo na kujua nini cha kwenda kufanya kuhusu agenda ya mazingira”.

Amesema kuwa kutakuwa na kampeni kabambe itakayohusisha wadau mbalimbali wa maendeleo lengo likiwa ni kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi ya mfano duniani katika utunzaji mazingira, “kampeni hii itakuwa endelevu, afua mbalimbali za mazingira zitaongeza thamani katika kampeni hiyo.”

Young Africans yabisha hodi KMC FC
Waziri wa Uganda apigwa risasi