Beki wa wana Jangwani, Young Africans Sports Club (Yanga), Kelvin Yondani ‘Vidic’ atakabidhiwa tena mikoba ya unahodha wa klabu hiyo iliyowekwa kando na Ibrahim Ajibu aliyetimkia Klabu ya Simba, kwa mujibu wa taarifa kutoka katika vyanzo vya ndani ya klabu hiyo.

Yondani anadaiwa kuwa chaguo la kocha Zahera ambaye Januari mwaka huu alitangaza kumvua kitambaa cha unahodha kwa sababu za utovu wa nidhamu na kumkabidhi Ajibu.

Endapo Kocha Mwinyi Zahera atatimiza kinachoelezwa na vyanzo hivyo, atakuwa amempa nafasi Yondani kuwa nahodha kwa kipindi cha muda mrefu ingawa sio cha muendelezo.

Yondani ambaye aliwahi pia kukipiga katika klabu ya Simba alikabidhiwa kitambaa cha unahodha wa Yanga kutoka kwa kaka yake, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ambaye alitundika daruga.

Ajibu aliyetimkia Simba, aliwahi kueleza kuwa hakuwa na furaha aliyoitamani ndani ya klabu hiyo ya Jangwani na ndio sababu alifikiria kutua Msimbazi; na hivi karibuni yametimia.

Julius Mtatiro ateuliwa kuwa DC wa Tunduru
Chadema watangaza kutinga mahakamani kudai ubunge wa Lissu