Baada ya mapumziko wakubwa wanarudi tena viwanjani. Huenda kuna ugumu wakaupata katika mechi zao za leo, kutokana na kulikosa joto la michezo ya ligi kwa wiki mbili, tofauti na wapinzani wao.

Young Africans watakuwa Uhuru, Dar es Salaam dhidi ya Polisi, Simba watakuwa Nelson Mandela, Sumbawanga dhidi ya Prisons.

Young Africans VS Polisi Tanzania

Sitarajii kuona mbinu za Cedric Kaze katika mechi hii, zaidi nitaziona mbinu za Mwambusi zikienda kuiamua mechi, japo waliindaa pamoja timu ya kucheza mechi hii.

Ugeni, muda mfupi kazini ni vitu viwili  vitakavyomfanya Kaze awe mtazamaji zaidi, sio mtendaji katika mechi hii. Baada ya dk 90 za mchezo huu kuna picha ya ligi yetu ataipata.

Young Africans ina changamoto ya kukosa Pira Biriani, lakini wana uhakika wa kupata ushindi kwa % 98. Wametuonyesha hili katika mechi zao 5 walizocheza mpaka sasa.

Wanakosa muunganiko wa kitimu, lakini kiwanjani wana watu wanaoweza kuwapa pointi tatu. Mara kadhaa Mukoko, Lamine wameziamua mechi.

Ditram Nchimbi atakuja katika mechi hii akiwa na kumbukumbu nzuri. Msimu uliopita aliitumia mechi hii alipokuwa Polisi kuiadhibu Yanga. Aliondoka kiwanjani kama shujaa kwa kupiga Hatrick. Baadae Yanga wakamsajili.

Polisi wanaweza kuutumia mwanya wa Yanga kujitafuta, wao wakapata pointi 3,1. Lakini ili kupata pointi 3,1 za Yanga wanatakiwa kukimbia sana kiwanjani.

Tanzania Prisons Vs Simba SC.

Mechi nyingine ngumu inayopigwa katika kiwanja kigumu. Simba ‘Kibubutu’ dhidi ya Prisons iliyoipania mechi.

Simba SC watawakosa Chama, Bwalya, Kagere,  Bocco, Fraga, lakini wana kikosi cha kuifanya Prisons ikutane na ugumu kiwanjani.

Nahodha wa Prsons Benjamin Asukile alisema halijui vyema jina la Miquessone, lakini leo atalijua vyema kama Miquessone atakuwa ameamka katika ubora wake.

Prisons ni wagumu. Ugumu wao unakolezwa na safu yao ya ngumu ya ulinzi chini ya Majemedari Asukile, Vedastus Mhambi, Nurdin Chona na juu yao Jumanne Elfadhil.

Kubwa kabisa Mugalu awe mvumilivu wa ‘mateke’ ya kina Mhambi. Wanaume wale hawana mzaha. Lakini Mugalu mwenyewe sio lele mama. Anaweza kuminyana.

Imeandaliwa na Abdul Mkeyenge.

Marekani yawatuhumu Urusi na Iran kuingilia uchaguzi
RC Dar awataka wananchi kulinda amani kipindi cha uchaguzi