Wanachama wa Yanga wamekubali kumkodisha klabu hiyo Mwenyekiti wao, Yusuf Manji kwa miaka 10 kuanzia leo.

Uamuzi huo umefikiwa katika Mkutano Mkuu wa dharula uliofanyika leo ukumbi wa Diamond jubilee, Dar es Salaam.

Manji ameomba apewe klabu kwa miaka 10 na katika kipindi hicho atakuwa anachukua asilimia 75 ya mapato ya timu, huku asilimia 25 ikibaki kwa wanachama.

Na katika kipindi hicho cha miaka 10, timu ya soka na nembo ya klabu zote zitakuwa chini ya Manji. Aidha, Mjumbe wa Baraza la Wadhamini la klabu, Francis Kifukwe alisema baada ya wanachama kuridhia mpango huo, wao wanampa pia ridhaa hiyo Manji.

Katika mkutano huo pia wanachama watatu wa klabu hiyo, Ayoub Nyenzi, Salum Mkemi na Hashim Abdallah walifukuzwa.

Manji aliwaambia wanachama hayuko tayari kufanya kazi na Wajumbe hao wa Kamati ya Utendaji na akaomba wanachama wanaowataka wajitokeze kupiga kura, lakini hakuna aliyeinuka.

Baada ya kurudia kuita mara tatu, Hashim pekee kati ya watatu hao ambaye alikuwepo mkutanoni ukumbi wa Diamond Jubilee, akainuka na kuondoka.

Mwanachama mwingine, Siza Lyimo ambaye Manji alitaka aondoke, yeye aliomba msamaha na wanachama wakamsamehe na Mwenyekiti huyo akabariki msamaha huo.

Mkemi na Nyenzi hawakutokea kwenye Mkutano huo.

Mtibwa Sugar Waibana Young Africans
Makonda aandaa ‘matrekta’ kubomoa UKUTA wa Chadema