Kaimu Kocha Mkuu wa Simba SC ni kama ameutega Uongozi wa Klabu hiyo, katika kipindi hiki ambacho wanamsaka Kocha Mkuu atakayekabidhiwa kikosi kwa ajili ya maandalizi ya msimu ujao 2024/25.

Mgunda alitangazwa kukaimu nafasi ya Kocha Mkuu klabuni hapo, kufuatia uongozi wa Klabu hiyo kuvunja mkataba na Kocha Benchikha aliyeondoka nchini kwa sababu za kifamilia.

Baadhi ya Mashabiki na Wanachama wa Simba SC wamekuwa wakiutaka Uongozi wa klabu hiyo kumkabidhi Mgunda majukumu ya kocha Mkuu, kwani amekuwa na msaada mkubwa klabuni hapo kila anapokaimu nafasi hiyo.

Mgunda amesema kwa sasa anachofanya ni kutimiza wajibu wa kuiwezesha timu ya Simba kufikia malengo ya kupambana uwanjani na kupata matokeo mazuri, lakini mambo mengine anawaachia viongozi wake wataamua.

“Nimepewa jukumu la kufundisha Simba SC na kazi yangu ni kufundisha, ndio majukumu niliyopewa na viongozi wangu, hawa mengine tusubiri ligi itakapomalizika tutafanya tathmini kwa pamoja kwamba baada ya hii kazi niliyopewa nini nimekifanya na nini kimepatikana na nini muendelezo wangu.” amesema Mgunda

Tangu alipokabidhiwa nafasi ya kukaimu kama Kocha Mkuu, Mgunda ameshinda michezo mitatu mfululizo dhidi ya Mtibwa Sugar (2-0), Tabora United (2-0) na Azam FC (3-0), huku akiambulia sare ya 2-2 dhidi ya Namungo FC.

Zaidi ya 49 wapatiwa huduma za kibingwa Tanganyika
Zanzibar, Bara kushirikiana ujenzi wa Miradi