Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Bukombe mkoani Geita, Dkt. Doto Biteko amewahimiza wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanapata elimu kwa kuwa ndio nguzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Dkt. Biteko amesema hayo wakati akihutubia mkutano wa wananchi katika Shule ya Msingi Bufanka iliyopo Kijiji cha Bufanka, Kata ya Bugelenga, Jimbo la Bukombe mkoani Geita.

Amesema, “naona aibu kuona watoto wanazuiwa wasiende shule, niwaombe wazazi tupeleke watoto shule. Wenyeviti wa Vijiji niwaombe kama kuna mtoto kwenye kijiji chako ambaye anatakiwa kwenda shule na haendi, nenda kwenye kaya hiyo kuwaeleza kuhusu umuhimu wa elimu ili mtoto huyo aweze kwenda shule.”

Dkt. Biteko ameongeza kuwa, Serikali imeendelea kujenga shule ambapo kwa sasa Wilaya ya Bukombe ina shule za Sekondari 7 na shule 5 za kidato cha tano na sita, huku akichangia ujenzi wa madarasa ya shule iliyopo katika Kata ya Bugelenga kwa kutoa mabati 135 na mifuko 400 ya saruji kwa ajili ya ukamilishaji wa miradi mbalimbali.

Katika hatua nyingine, Dkt. Doto Biteko amewataka Wananchi wa Kijiji cha Bufanka na Jimbo la Bukombe kujiandaa kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika mwaka huu kwa kuchagua viongozi wenye sifa watakaosaidia kuleta maendeleo.

“Viongozi wa Chama chetu na Katibu Kata anzeni kwenda kwenye kata zetu kuwaambia mabalozi tukutane ili tujadiliane kuhusu uchaguzi, watu wengine wanashangaa Chama Cha Mapinduzi kinashindaje, wajue tu ni kwa kuwa tunajipanga mapema kwa ajili ya kesho.” Amesema Dkt. Biteko.

Naye, Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Festo Dugange amesema kuwa Dkt. Biteko amesemea miradi mingi kwa ajili ya kuwasaidia wananchi na Rais Samia ametoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya na zahanati.

“Hapo awali huduma zilikuwa mbali na gharama za kwenda kupata matibabu zilikuwa juu kakini Mhe. Dkt. Biteko aliona changamoto hiyo na alipomueleza Mhe. Rais Samia Wilaya hii ilipewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya kutatua changamoto hiyo”, amesema Mhe. Dugange.

Akizungumzia daraja lililopo mpakani kati ya Bugelenga na Mbogo, Dugange amesema “ Serikali tayari imetenga shilingi milioni 585 kwa ajili ya ujenzi wa daraja, na shilingi milioni 85 zimeshaletwa hapa, TARURA wataanza kutafuta mkandarasi na katika kipindi cha ndani ya mwezi mmoja na nusu ujenzi wa daraja hili utaanza na baadaye tutaanza ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita 30.”

Kuhusu sekta ya elimu, amesema kuwa ndani ya kipindi cha miaka minne Jimbo hilo limepata zaidi ya shilingi bilioni 9 kwa ajili ya miradi ya ujenzi wa shule za msingi na sekondari. Aidha, amewapongeza wananchi kwa kuwa na mbunge hodari, mchapakazi na mwenye kujali na kutatua changamoto zao.

Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Geita, Nicholaus Kasendamila amemshukuru Dkt. Biteko kwa kuendelea kuwasaidia wananchi wa Bukombe kwa kuhakikisha wanapata maendeleo kwa kuwa na miradi mbalimbali ikiwemo ya shule, hospitali na barabara.

Aidha, amewasihi wananchi wa Bukombe kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa “Huu ni mwaka wa uchaguzi tunatakiwa kujiandaa na viongozi wa CCM katika Mkoa huo tuhamasishe wapiga kura kushiriki katika uchaguzi na hatimaye kuchagua viongozi wazuri.”

Kwa upande wake, Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa wa Geita, Rose Busiga amesema kuwa Mbunge wa Jimbo hilo Dkt. Doto Biteko ameendelea kutatua changamoto zao mbalimbali ikiwemo ya mawasiliano na tayari fedha za kujenga minara 9 ya mawasiliano zimeshaletwa jimboni.

Sheria: TVLA yawataka Wazalishaji Vyakula vya Mifugo kuhakiki ubora
Ubovu wa Barabara: Wananchi wafunga njia Moro