Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka wamiliki wa malori nchini wawajali madereva na wahudumu wa magari hayo ikiwa ni pamoja na kuboresha maslahi yao na kwamba uanzishwaji wa kanzidata ya taarifa za madereva utawawezesha wamiliki kutumia taarifa hizo kwa lengo la kusimamia usalama wa madereva pamoja na kufuatilia mienendo na ufanisi wao.

Majaliwa ameyasema hayo, akizungumza na wadau wa sekta ya usafirishaji waliohudhuria uzinduzi wa kanzidata ya madereva wa malori nchini leo (Alhamisi, Desemba 14, 2023) jijini Dar es Salaam. Kanzidata hiyo imeandaliwa na Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (TATOA).

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Amesema, “katika hili, niwasisitize kuhusu kuzingatia usalama na maslahi ya madereva wenu ambao kimsingi ni walinzi wa mitaji yenu kupitia vyombo ambavyo mmewapa dhamana ya kuviendesha. Haki iende na wajibu, yaani mnataka wawatumikie, kwa hiyo na ninyi mboreshe maslahi yao.”

Akizungumza na wadau wa sekta hiyo, Waziri Mkuu amesema azma ya Serikali ya awamu ya sita ni kuendeleza sekta hiyo ili iweze kuharakisha ukuaji wa uchumi. “Hatua iliyofikiwa leo ni kuhakikisha makao makuu ya mikoa yote inafikika kwa lami na shoroba zote za Kusini, Kati na Kaskazini kuelekea nchi za jirani za Kenya, Kongo, Malawi na Zambia zinapitika bila shida.”

Akielezea maboresho ya sekta hiyo, Waziri Mkuu amesema Serikali tayari imekamilisha ujenzi wa barabara za lami zenye urefu wa km. 2,183.82 na km. 14,348 za changarawe. Licha ya hayo imekuwa ikiendelea na matengenezo ya kawaida ili kuzifanya barabara zetu ziweze kupitika wakati wote.

Sambamba na maboresho hayo ya barabara, Waziri Mku amesema Serikali inaendelea na ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa (SGR) unaoambatana na uundaji wa vichwa 17 vya treni, uboreshaji wa bandari za Dar es Salaam, Mtwara, Tanga na kwenye maziwa makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa ambapo muda wa kugomboa mizigo bandarini umepungua kutoka siku 14 hadi siku sita.

Nsajigwa, Niyonkuru waachiwa msala Namungo
Uwajibikaji: Tumieni hekima, tendeni haki - ACP Mchunguzi