Timu za Maafande zitakazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao 2023/24 Tanzania Prisons na JKT Tanzania zimepanga kuweka kambi nchini Tanzania ili kujiweka tayari na msimu huo, ambao unatabiriwa kuwa na ushindani wa vuta nikuvute.

Taarifa zilizopatikana kutoka Jijini Mbeya zinaeleza kuwa Tanzania Prisons imepanga kwenda kujifua visiwani Zanzibar kwa muda wa mwezi mmoja na Afisa Habari wa timu hiyo, Jackson Mwafulango amesema mapendekezo hayo ni ya Benchi la Ufundi kwani wanaamini huko ni sehemu tulivu na salama kuweka kambi.

“Kuanzia wiki ijayo tunatarajia kwenda huko na baada ya hapo kama ilivyo utaratibu wa kila msimu mpya lazima tutafute michezo ya kirafiki ambayo itatupa mwanga mzima wa kikosi chetu,” amesema Mwafulango huku kocha wa kikosi hicho Abdallah Mohamed “Bares akisema, wao kama benchi la ufundi wamepanga kuanza kambi mapema ili kupata muda mrefu wa kujiandaa vyema.

“Tumeanza mazoezi rasmi leo  Jumatatu hapa jijini Mbeya na baada ya hapo tutaanza mipango ya kwenda Zanzibar ambako huko tutapata fursa nzuri ya kupata michezo mingi ya kirafiki,” amesema.

Wakati Prisons wakisema hivyo kwa upande wa JKT Tanzania iliyorejea Ligi Kuu Bara yenyewe imepanga kwenda Shinyanga.

JKT inayonolewa na kocha mzoefu, Malale Hamsini kambi yao itaanza Julai 10 mkoani humo, huku ikiendelea kufanya usajili wa kimyakimya.

Waliosajiliwa hadi sasa JKT Tanzania ni viungo wa Hassan Dilunga, Hassan Nassoro ‘Machezo, Deusdedith Okoyo, Ismael Aziz Kader, sambamba na beki George Wawa na washambuliaji Tariq Seif na Danny Lyanga.

TPSF, UDSM wasaini MOU ajira za Wahitimu wa Vyuo
Kijana amuuwa bibi kwa panga, kisa kinashangaza