Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini imeahidi kutimiza ahadi ilizozitoa wakati wa kampeni kwa wachimbaji wadogo wadogo wa madini na kusema kuwa muda wa kula matunda ya kazi hiyo umewadia.
 
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo alipokuwa akizungumza na wachimbaji wadogo wadogo wa madini ya dhahabu katika eneo la kitunda wilayani Sikonge mkoani Tabora, amesema kuwa sasa ni vyema kuhakikisha wachimbaji hao wanatoa ajira kwa wingi kwa wanachi waliopo katika eneo hilo.
 
Amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano iliahidi wakati ikiomba kura kwa wananchi kuwashika mkono wachimbaji wadogo wadogo na kwa kuwa neema hiyo sasa imepatikana hapo ni vema vijana wengi wa eneo hilo wenye nia ya kushiriki katika uchimbaji wa madini wakanufaika na ajira.
 
“Kila mgodi uwe na majina ya watu wanaotaka kuwaajiri na orodha hiyo ifike kwa Mkuu wa Mkoa , Maafisa wa Madini wa Kanda ikiwa imeonyesha jina la kila moja na idadi yao, hatuwezi kuwacha vijana hawa wote bila ajira,”amesema Muhongo.
 
Aidha, hatua hiyo imelenga kuondoa tabia ya baadhi ya wachimbaji hao kuvamia maeneo ya wengine na hivyo kuhatarisha maisha yao naya wengine.
 
Kwa upande wake Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda Kati Magharibi Salim Salim amesema kuwa ili kuhakikisha maafa mengine hayatokei, kabla ya kuanza tena uchimbaji katika eneo hilo Ofisi ya Kanda kwa kushirikiana na Afisa Mkazi wa Madini wameshaanza kusimamia zoezi la kuhakikisha mashimo ya uchimbaji wa dhahabu yanakuwa kuanzia mita 15 toka moja kwenda jingine.

Video: Serikali kuwalipa fidia wakazi wa kipunguni
Video: Majaliwa aongoza mazishi ya diwani wake Ruangwa