Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewataka watanzania kuendelea kuchukua tahadhari juu ya tishio la ugonjwa wa Ebola.

Rais Samia amesema hayo leo Oktoba 14, 2022 mjini Bukoba mkoani Kagera katika maadhimisho ya kilele cha mbio za mwenge wa Uhuru kitaifa yaliyokwenda sambamba na kumbukizi ya miaka 23 ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Amesema, “Tumekumbana na changamoto za maradhi mbalimbali ikiwemo corona tumepita ,sasa kuna Ebola japo haijatufikia hivyo watanzania tuendelee kuchukua tahadhari dhidi ya Ebola.”

Rais Samia amesema suala la afya ya binadamu huendana na lishe bora huku akiipongeza Wizara ya Afya kwa kuendelea kutoa elimu ya lishe kwa jamii na kusisitiza jitihada za mapambano dhidi ya malaria ili kupunguza vifo vya mama na mtoto.

Amefafanua kuwa, “Kiwango cha maambukizi ya Malaria kimepungua kwa 14.8% mwaka 2015 hadi kufikia 7.3% mwaka 2017, na ugonjwa huu bado ni changamoto kwa watoto wa umri chini ya miaka mitano na kwa akina mama wajawazito maambukizi bado ni makubwa kwa baadhi ya mikoa.”

Kuhusu ugonjwa wa UKIMWI, Rais Samia amesema maambukizi bado yapo na yanapoteza nguvu kazi ya taifa hasa kwa vijana na akasema “Takwimu zinasema hadi kufikia mwaka 2021 asilimia 88 ya watu walikuwa wanajitambua hali zao na asilimia 89 wakiwa kwenye tiba.

Waganda walia na Museveni sheria mpya ya mtandao
Truss ajiweka pabaya kumfuta kazi Kwarteng