Baada ya kuchomoza na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Primeiro De Agosto ya Angola jana Jumapili (Oktoba 09), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Simba SC Salim Abdallah ‘Try Again’ amewahimiza Mashabiki na Wanachama wa klabu hiyo kuendelea kuwa kitu kimoja katika kipindi hiki.

‘Try Again’ amesema Umoja na Mshikamano baina ya Wanachama na Mashabiki ndivyo vitakavyoweza kuivusha timu yao hadi hatua ya Makundi, kwa kuhakikisha wanashinda mchezo wa Mkondo wa Pili utakaopigwa na Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam Jumapili (Oktoba 16).

Kiongozi huyo amesema bado Simba SC ina kazi ya kupambana kwenye mchezo wa pili dhidi ya Primeiro De Agosto, na ana imani kubwa Wachezaji watamalizia kazi walioianza ugenini jana Jumapili (Oktoba 09).

“Imekua furaha kwa kila Mwanasimba kwa ushindi huu, ninawasihi Wanasimba wote kuendelea kuwa kitu kimoja naamini tukiwa katika hali hii tutafanikiwa na kushinda tena katika mchezo wa Mkondo wa Pili utakaochezwa Dar es salaam.”

“Ushindi huu naamini umepatikana kutokana na Mshikamano wetu ambao siku zote umekua kama silaha ya kuwaangamiza wapinzani, nina uhakika tukifanikisha hili hata ule mchezo wa Dabi tutaingia tukiwa na matumaini ya kuendeleza furaha yetu ya ushindi.” amesema Try Again

Tayari kikosi cha Simba SC kimeshawasili jijini Dar es salaam majira ya Alfajiri kikitokea Luanda-Angola kilipokuwa na kazi kubwa ya kuikabili Primeiro De Agosto.

Mgunda: Primeiro De Agost wasichukuwe poa
Dkt. Kikwete atoa neno maonesho Viwanda na Biashara